Breaking

Monday 28 November 2022

WAZIRI MKUU AKAGUA UJENZI DARAJA KIBITI, AWAPA MAAGIZO MAZITO WAKUU WA MIKOA, WATUMISHI HALMASHAURI




Wakazi wa Kata za Mbuchi na Mbwera Kibiti Mkoani Pwani wamemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan kwa ujenzi wa daraja la Mbuchi linalounganisha kata hizo ambalo limegharimu shilingi bilioni 7.2.

Wamezungumza hayo leo (Jumatatu, Novemba 28, 2022) wakati Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alipotembelea kukagua ujenzi wa daraja hilo lenye urefu wa mita 61.



Wakizumgumza kwa nyakati tofauti wananchi hao wamesema kuwa ujenzi wa daraja hilo umesaidia kwa kiasi kikubwa kuondoa adha ya usafiri kati ya kata hizo ambapo awali iliwalazimu kutumia mitubwi ambayo ilikuwa tishio kwa uhai wa wakazi hao hasa kipindi cha mvua kubwa mto huo ukiwa imejaa.

“Sisi kina mama tuliteseka kwa muda mrefu sana, safari za kwenda kufuata huduma za afya kwetu ilikuwa ni mtihani mkubwa, tulihofia maisha yetu, lakini kwasasa hata usiku wa manane tunavuka bila shida kufuata huduma za afya, tunamshukuru sana Rais wetu kwa kuiona changamoto yetu na kuifanyia kazi”


Akizungumza na wananchi baada ya kukagua ujenzi wa daraja hilo, Mheshimiwa Majaliwa amewataka wakazi hao kulitumia daraja hilo kujiimarisha kiuchumi kwa kujishughulisha na kazi mbalimbali kwakuwa usafiri kwenye eneo hilo umekuwa wa uhakika kwa muda wote.

Aidha, Waziri Mkuu amewataka wakazi hao kuwa walinzi namba moja wa miundombinu kwenye daraja hilo ili iweze kudumu kwa muda mrefu na kutekeleza malengo yaliyokusudiwa ya ujenzi wa daraja hilo.

Kwa upande Mwingine, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ameagiza viongozi wa mikoa kuhakikisha wanachukua hatua za kisheria mfugaji ambaye ameshindwa kufuata Sheria za nchi na kuamua kulisha mifugo kwenye mashamba ya wakulima.

Pia Waziri Mkuu alitembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa hospitali ya wilaya ya kibiti ambapo awamu ya kwanza ilihusisha ujenzi wa majengo saba ikiwemo jengo la utawala, wagonjwa wa nje, maabara, wazazi, jengo la kufulia na jengo la stoo ya dawa ambapo ujenzi wa mradi huo umegharimu shilingi bilioni 1.8.

Amesema kuwa Serikali ya awamu ya sita inathamini na kuwajali wafugaji nchini kwa kuwa sekta ya mifugo inatija kwenye uchumi wa nchi ikiwemo kuleta fedha za kigeni lakini ni lazima wafugaji wazingatie sheria.

Akizungumza na Watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti, Mheshimiwa Majaliwa amewataka wakuu wa idara kwenye Halmshauri wahakikishe kila eneo wanalosimamia linafanya kazi kwa ufanisi na kuleta matokea serikalini

Pia amewataka watumishi hao wahakikishe wanawahudumia wakulima katika maeneo mbalimbali katika wilaya hiyo kwakuwa kuna idadi kubwa ya wakulima ili shughuli zao ziweze kuleta tija na kukuza uchumi wao na taifa kwa ujumla.

Kwa upande Naibu Waziri Ofisi ya Rais TAMISEMI Dkt. Festo Dugange amesema kuwa ujenzi wa daraja hilo umewezesha wakazi wa kata hizo kupata huduma za afya katika kituo kipya cha afya cha mbwera ambacho kimekuwa mkombozi kwa wananchi wa kata hizo.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages