Breaking

Thursday 3 March 2022

WAKIMBIZI KUTOKA UKRAINE WAFIKA MILIONI 1, ZAIDI YA 2000 WAUAWA KATIKA MAPIGANO NA URUSI



Na Samir Salum 

Takwimu za Umoja wa Mataifa zimebaini kuwa idadi ya wakimbizi wanaokimbia mzozo wa Ukraine imeongeza na kufikia zaidi ya milioni moja tangu Urusi ilipovamia nchi hiyo.

Kamishna Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa Shirika linalohudumia Wakimbizi UNHCR, Filippo Grandi, katika chapisho la Twitter alilochapisha mapema leo Alhamisi Machi 03, 2022 amesema kuwa Katika muda wa siku saba tu  wakimbizi milioni moja kutoka Ukraine wamekimbilia nchi jirani.

 "Kwa mamilioni zaidi, ndani ya Ukraine, ni wakati wa bunduki kunyamaza, ili msaada wa kibinadamu wa kuokoa maisha uweze kutolewa." Amesisitiza Grandi



 Kwa mujibu wa shirika la umoja huo linalowahudumia wakimbizi UNHCR imesema  kuwa idadi hiyo ni ongezeko la wakimbizi takriban 400,000 kutoka kwa 877,000 iliyotangazwa na mkuu wa shirika hilo Filippo Grandi kiasi saa 24 kabla.

UNHCR imesema mzozo wa Ukraine umesababisha uharibifu na miundombinu ya umma, vifo na majeraha ya raia na kuwalazimu maalfu ya watu kuyakimbia makazi yao.

Shirika hilo linakadiria zaidi ya wakimbizi milioni nne raia wa Ukraine huenda hatimaye wakahitaji ulinzi na msaada.

Umoja wa Mataifa  Jumanne Machi Mosi ulizindua mchango wa dola bilioni 1.7 kwa ajili ya msaada wa dharura wa kiutu kwa watu walionasa katika uvamizi wa Urusi na kwa wakimbizi wanaokimbia machafuko.

Aidha Mamlaka nchini Ukraine zinasema kuwa zaidi ya raia 2,000 wameuawa kufikia jana Jumatano Machi 02, 2022 katika uvamizi wa Urusi, ambao ulianza karibu wiki moja iliopita.

Waokoaji wamezima moto zaidi ya mara 400 uliozuka baada ya makombora ya Urusi kote nchini na kuzima vilipuzi 416.

"Kufuatia siku saba za vita, Urusi imeharibu mamia ya vituo vya usafiri, majengo ya makazi, hospitali na shule za chekechea," ilisema.

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages