Breaking

Monday 18 April 2022

WAZIRI DKT. GWAJIMA ATAJA NAMBA KUWEZESHA UTOAJI TAARIFA KUPAMBANA NA UKATILI

Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia Wanawake na Makundi Maaalum Dkt. Dorothy Gwajima akiongea na wananchi wa kata ya Chamazi, alipofanya ziara fupi kwenye Kata hiyo leo Aprili 18,2022.

Afisa Ustawi wa Jamii, Manispaa ya Temeke akimkabidhi Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia Wanawake na Makundi Maaalum Dkt. Dorothy Gwajima taarifa ya utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto (MTAKUWWA) ya Halmashauri hiyo.

Diwani wa Kata ya Chamazi jijini Dar es Salaam Lawrence Gama, akiongea wakati wa ziara ya Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia Wanawake na Makundi Maaalum Dkt. Dorothy Gwajima kwenye kata hiyo leo Aprili 18,2022.

Wananchi wa Kata ya Chamazi katika Manispaa ya Temeke, wakimsikiliza Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia Wanawake na Makundi Maaalum Dkt. Dorothy Gwajima alipofanya ziara katika kata hiyo leo Aprili 18,2022.

Kamishna Msaidizi wa Ustawi wa Jamii Baraka Makona akizungumza na wananchi wa Kata ya Chamazi mara baada ya Waziri wa Maendeleo ya Jamii,Jinsia, Wanawake na Makundi Maaalum Dkt. Dorothy Gwajima kufanya ziara katika Kata hiyo, leo Aprili 18,2022.

Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia Wanawake na Makundi Maaalum Dkt Dorothy Gwajima katika picha ya pamoja na Kamati ya Ulinzi wa Wanawake na Watoto (MTAKUWWA) mara baada ya Waziri huyo kufanya ziara katika kata ya Chamazi Jijini Dar es Salaam leo Aprili 18,2022.

Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia Wanawake na Makundi Maaalum Dkt Dorothy Gwajima akiwa na Mtoto (Matumaini), miaka 15 'sio jina lake halisi' aliyefunikwa ambaye ni Mnusurika wa kuolewa

***************

Na Mwandishi Wetu-Dar Es Salaam


Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima, amezitaja namba za simu rasmi  kuwawezesha wananchi kutoa taarifa pindi wanapoona vitendo au viashiria vya ukatili ili kuweza kuikomboa jamii na vitendo hivyo.


Hatua hiyo ya Dkt. Gwajima, imefuatia ziara yake katika Kata ya Chamazi, Wilaya ya Temeke, mkoani Dar es salaam, leo Aprili 18, 2022.


Akizungumza katika eneo hilo, Dkt. Gwajima, amesema matukio kama ya binti mwenye umri wa miaka 15 kutaka kuozeshwa na mengine mengi ndio kiini kilichowasukuma kuja na mkakati huo ili kila mmoja ndani ya jamii aweze kuwa mlinzi ndani ya jamii.


“Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009 kifungu cha 95, kinamlinda mtoto dhidi ya madhila kama haya, lakini kama haitoshi sheria ya elimu ya mwaka 1978 na maboresho yake ya mwaka 2016, vinasema waziwazi ni marufuku kwa mtoto kuozeshwa akiwa bado anasoma, lakini hata wale wanaoshuhudia kitendo hicho huweza kukumbwa na sheria hiyo” alisema Dkt. Gwajima.


Amefafanua kuwa kwakuwa binti huyo alikuwa bado ni mwananfunzi na Serikali ya Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa sasa inatoa elimu bila malipo amewataka wazazi kumrudishia mtoto huyu kuendelea na masomo na kusema hatua ya kuja na mkakati wa kutangaza namba hizo ni muhimu ili watoto waweze kufikia ndoto zao. 


Dkt. Gwajima amezitaja namba hizo kuwa ni namba 116 ambayo ni namba ya bure, lakini pia ametoa namba yake kwa jamii ya 0734-124191 kwa ajili ya kuandika ujumbe mfupi wa maandishi sambamba pia na namba za Kamanda Mkuu wa Dawati la Jinsia la Polisi Makao Makuu 0784-484731 lakini pia wataalam wa Ustawi wa Jamii ngazi zote kuanzia Taifa, Mkoa hadi kwenye Halmashauri.


“Tumeanza kwakutoa namba ambazo tumeziweka kwenye tovuti, na Mitandao yetu ya kijamii, lakini shabaha yetu ni kila mwanajamii aweze kuzipata namba hizi sehemu yoyote ikiwepo wenzetu wa vyombo vya Habari watusaidie katika hili kufikisha ujumbe huu” amesisitiza Dkt. Gwajima.


Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Kamishna Msaidizi wa Ustawi wa Jamii kutoka kwenye Wizara hiyo Baraka Makona, alisema kutolewa kwa namba hizo ni ishara kwamba Wizara hiyo ipo kazini na muda si mrefu Wizara itatoa namba za Maafisa Ustawi wa Jamii wote waliopo ngazi ya Halmashauri, na namba hizo zitakuwa tunaziuhuisha kadri siku zinavyo kwenda.


"Watu wakatili wajue kabisa Serikali na Jamii ya watu wapenda amani tupo kazini tutapokeantaarufa za vitendo vya ukatili na kuzifabyia kazi kwa kushirikiana na Mamlaka nyingine” alisema Baraka.


Kwa Upande wake Mkurugenzi wa Manispaa ya Temeke Elihuruma Mabelya, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi wa  Mwanamke na Mtoto wa Manispaa hiyo, amempongeza Waziri kwa kuwa na sikio la haraka na wepesi wa kufatilia suala la Ukatili hasa kwa Wanawake na Watoto kwani vitendo hivyo vimekithiri katika jamii vinaitwji kuqngaliwa kwa namna ya kipekee ili kuvitokomeza.


“Sote tunafahamu kuwa leo ni jumatatu ya pasaka, lakini kwa kuguswa kama mama, ameona ni vema afike kumuona binti huyu ambaye alikuwa aozeshwe kutokana na migogoro ya familia, ambayo ilimsababisha binti akaona bora aolewe, kitendo hiki kwakweli sio kizuri, hivyo tunampongeza sana Waziri Dkt. Gwajima" alisema Mabelya.


Awali akitoa taarifa ya masuala ya Ukatili kwenye Manispaa hiyo, Afisa Ustawi wa Jamii wa Manispaa ya Temeke Lilian Mafole, alisema, siku ya tukio walipokea taarifa ya kutaka kuozwa kwa binti huyo ndipo wakajikusanya kuanzia ngazi ya Manispaa, Kata na Mtaa husika huku wakiwa wameweka mtego uliofanikisha kukamatwa kwa mtuhumiwa akiwa mbioni kufungishwa ndoa na Binti huyo.


Katika hatua Nyingine Dkt. Gwajima, akiwa kwenye ziara hiyo amefika kutoa pole kwa ndugu na Jamaa wa Mtoto anayekadiriwa kuwa na umri wa mika 4 (jina limehifadhiwa) ambaye alifanyiwa kitendo cha ukatili wa kulawitiwa na Baba mzazi, ambapo Waziri aliambiwa kuwa, shauri la mhusika tayari limefikishwa Mahakamani na hatua  za kisheria zinaendelea.


MWISHO

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages