Breaking

Monday 6 June 2022

CDF MABEYO KUSTAAFU MWEZI HUU, RAIS DKT. MWINYI AMPONGEZA



Na Samir Salum, Lango la habari

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Hussein Ali Mwinyi amempongeza Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Tanzania, Jenerali Venance Mabeyo kwa kutekeleza vyema majukumu yake katika kipindi chake chote cha utumishi ndani ya Jeshi hilo.


Kupitia taarifa iliyotolewa leo Jumatatu Juni 06, 2022 Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Charles Hilaly imeeleza kuwa Rais Dk. Mwinyi ametoa pongezi hizo wakati akizungumza na Jenerali Mabeyo ambaye alifika Ikulu Zanzibar kumuaga kufuatia kumaliza muda wa utumishi wake ndani ya Jeshi mwisho wa mwezi wa sita kwa mujibu wa sheria.



Amesema kuwa Jenerali Mabeyo ni kiongozi ambaye alifanya kazi zake vema katika Jeshi hilo na alimpa ushirikiano mkubwa yeye na viongozi wenzake wakati akiwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa hatua ambayo ilimuwezesha kutekeleza mabadiliko mengi ndani ya Jeshi hilo.


Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amemtakia kila la heri Jenerali Mabeyo katika maisha yake ya kustaafu hasa ikikumbukwa amelitumikia kwa muda mrefu Jeshi hilo na kufanya mambo mengi yatakayoacha alama.


Kwa upande wake Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Jenerali Mabeyo amempongeza na kumshukuru Rais Dkt.Mwinyi kwa kutekeleza vema uongozi wake tangu alipokuwa Waziri wa Ulinzi hadi hivi sasa ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.

Amesema Jeshi la Wananchi wa Tanzania litaendelea kumkumbuka Rais Dkt. Mwinyi kwa busara na hekima zake katika kuzishughulikia changamoto mbalimbali ndani ya Jeshi hilo ambalo hatimae limepata mafanikio makubwa.


Jenerali Mabeyo alisema Jeshi la Ulinzi Tanzania litaendelea kumkumbuka Rais Dk. Mwinyi kwa busara na hekima zake katika kuzishughulikia changamoto mbalimbali ndani ya Jeshi hilo ambalo hatimae limepata mafanikio makubwa.


Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Tanzania, Jenerali Venance Mabeyo baada ya kulitumia Jeshi kwa nafasi mbalimbali kuanzia 1 Januari 1979, mwishoni mwa mwezi huu atastaafu utumishi ndani ya jeshi hilo ambapo Nafasi ya CDF alianza kuitumikia 6 Februari 2017.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages