Breaking

Wednesday 22 June 2022

FIFA YAIFUNGIA BIASHARA UNITED KUFANYA USAJILI



Na Said Muhibu, Lango La Habari


Kamati ya nidhamu ya Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) imeifungia klabu ya ligi kuu Tanzania NBC Biashara United ya Mara kufanya usajili katika madirisha mawili.


Taarifa iliyotolewa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) leo June 22, 2022 imesema adhabu hiyo imekuja baada ya Biashara United kukiuka maagizo ya FIFA yaliyoielekeza klabu hiyo kukamilisha mishahara aliyokuwa akiidai mchezaji wao wa zamani Timoth Bolton Omwenga.


FIFA ilifikisha suala hilo kwenye kamati yake ya nidhamu mnamo Mei 19, 2022 ambayo ilitoa uamuzi huo kupitia kwa mjumbe wake Carlos Teran wa Venezuela.


Dirisha la kubwa la usajili kwa klabu za ligi kuu ya Tanzania NBC litafunguliwa Julai 1, 2022 na kufungwa Agosti 31, 2022 na dirisha dogo litafunguliwa Disemba 16, 2022 na kufungwa Januari 15, 2023.


Aidha, TFF imezishauri klabu za ligi kuu Tanzania NBC kuheshimu mikataba ambayo zinazoingia na wachezaji na makocha, kwani hiyo ni moja ya vigezo vya kupata leseni ikiwa ni kanuni ya utekelezaji wa leseni za klabu (Club License Regulations).

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages