Breaking

Tuesday 26 July 2022

CHANZO AJALI ILIYOUWA WATU 10 WAKIWEMO WANAFUNZI NANE MTWARA



Chanzo cha ajali iliyosababisha vifo vya watu 10 wakiwemo wanafunzi nane wa Shule ya Msingi ya King David ni gari kufeli kwa breki kisha kutumbukia shimoni.


Ajali hiyo imetokea asubuhi ya leo Jumanne, Julai 26, 2022 eneo la Mjimwema, Kata ya Mikindani, Mtwara Mjini wakati watoto hao wakitoka kuchukuliwa nyumbani kupelekwa shuleni.


Kaimu Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Mtwara, Nicodemus Katembo akizungumza na waandishi wa habari akiwa Hospitali ya Rufaa Ligula amesema, chanzo cha ajali hiyo ni kufeli kwa breki za gari iliyokuwa imewabeba wanafunzi hao.


Katembo amesema gari hiyo aina ya Hiace ilifeli breki na kumshinda dereva kisha kuingia kwenye mteremko na kusababisha wanafunzi nane na watu wazima wawili akiwemo dereva kufariki dunia na majeruhi zaidi ya 18.


Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Dk Hamad Nyembea amesema amepokea majeruhi 18 kati yao 12 ni wa kike na sita wa kiume.


Amesema majeruhi wanaendelea kupatiwa matibabu huku waliofariki wa kike ni watano, kiume ni watatu na watu wazima wawili.


Dk Nyembea amesema majetuhi watano wapo katika chumba cha uangaliazi maalum.


Kutokana na ajali hiyo, Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amewalilia wanafunzi hao akisema, “nimesikitishwa na vifo vya wanafunzi 8 wa Shule ya Msingi King David na watu wazima wawili vilivyotokea leo eneo la Mjimwema, Mikindani, mkoani Mtwara.”


“Natoa pole kwa wote waliopoteza jamaa zao. Mungu azilaze roho za marehemu mahali pema na awajalie majeruhi wapone haraka,” amesema Rais Samia kupitia akaunti yake ya twitter


Majira ya waliofariki na majeruhi hayajatajwa.


Endelea kutufuatilia kupitia mitandao yetu.


Source: Mwananchi
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages