Breaking

Wednesday 28 September 2022

TUME YA MADINI YAENDELEA KUWANOA WACHIMBAJI MAONESHO YA MADINI GEITA




Wataalam kutoka Tume ya Madini wameendelea kutoa elimu kwa wachimbaji wa madini kutoka katika mkoa wa Geita na mikoa ya jirani katika Maonesho ya Tano ya Kitaifa ya Teknolojia ya Madini yanayoendelea katika viwanja vya Bombambili mjini Geita .

Elimu imetolewa katika maeneo kadhaa ikiwa ni pamoja na fursa za uwekezaji katika sekta ya madini, taratibu za upatikanaji wa leseni za madini nchini, biashara ya madini na taratibu za usalama wa afya na mazingira kwenye migodi ya madini.

Maeneo mengine ni pamoja na namna watanzania wanaweza kushiriki katika Sekta ya Madini kupitia utoaji wa huduma mbalimbali kwenye migodi ya madini na mchango wa kampuni za uchimbaji wa madini kwenye jamii.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wananchi waliotembelea banda la Tume ya Madini wamepongeza weledi wa wataalam wa Tume ya Madini kwenye utoaji wa elimu na kuwaomba kuendelea na zoezi hilo katika mikoa mingine yenye shughuli za uchimbaji wa madini.

Akizungumza kwenye maonesho hayo, Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Tume ya Madini, Greyson Mwase amesema kuwa wamejipanga kutoa elimu kwa wadau wa madini na wananchi wote wanaotembelea maonesho hayo pamoja na huduma kama vile upimaji wa madini na kuwaelekeza namna ya kujisajili katika mtandao wa leseni za madini (online mining cadaster transactional porta).

“ Tumejikita pia kutoa elimu katika eneo la ushirikishwaji wa watanzania katika Sekta ya Madini (local content) ili wananchi wengi waweze kufahamu fursa zilizopo kwenye migodi ya madini na kuchangamkia kama vile utoaji wa huduma za vyakula, vifaa vya usalama migodini, ulinzi ili nao waweze kunufaika,” amesema Mwase

Ameendelea kusema kuwa Tume imeendelea kuweka mikakati mingine ya kuelimisha umma ikiwa ni pamoja na uandaaji na urushaji wa vipindi vya redio na televisheni, tovuti na mitandao ya kijamii.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages