Breaking

Wednesday 30 November 2022

TEITI YATAKIWA KUWEKA WAZI TAARIFA ZA MAPATO YA TASNIA YA UZIDUAJI




Taasisi ya Uhamasishaji Uwazi na Uwajibikaji Katika Rasilimali Madini, Mafuta na Gesi Asilia (TEITI) ina wajibu wa kuhakikisha mapato ya tasnia ya uziduaji yanahakikiwa na kutumika kwa manufaa ya wananchi ikiwemo jukumu la kuhakikisha Kampuni zinazofanya shughuli za utafutaji na uchimbaji wa Madini, Mafuta na Gesi Asilia zinaweka wazi taarifa za mapato.

Hayo yamebainishwa na Waziri wa Madini Dkt. Doto Biteko wakati akifungua Warsha ya Kuelimisha Madiwani, Asasi za Kiraia, Viongozi wa Halmashauri na Wachimbaji wa Madini juu ya matumizi ya takwimu zinazotolewa katika ripoti za TEITI iliyofanyika katika Ukumbi wa Mkuu wa Mkoa Songwe.

Aidha Dkt. Biteko amesema, tayari taarifa za TEITI zinahakikiwa na kutumika kwa manufaa ya wananchi wote na kielelezo kikubwa katika kufanikisha na kuboresha suala zima la uwazi na uwajibikaji katika sekta ya uziduaji Nchini.

"Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan ina dhamira ya dhati kuona sekta hii inawanufaisha watanzania wote kwa kuhakikisha kwamba Serikali inapata mapato stahiki na wananchi wanashiriki kikamilifu katika usimamizi wa rasilimali hizo na huku kampuni zinazofanya shughuli za utafiti na uchimbaji wa Madini, Mafuta na Gesi Asilia zinawajibika kuweka wazi taarifa za mapato yake kulingana na Sheria inavyoelekeza," amesema Dkt Biteko.

Ameongeza kuwa, uwepo wa taasisi ya TEITI nchini ni muhimu kwa maendeleo ya Taifa na wananchi ambapo ameeleza kuwa, ni matumaini yake kuwa wadau kupitia fursa hiyo watajifunza na kuibua mijadala ambayo itasaidia kuboresha sekta hiyo ikiwemo ushiriki wa wananchi katika kutoa huduma na bidhaa kwenye migodi.

Pia, Dkt. Biteko amesema warsha hiyo itasaidia kuelimisha washiriki juu ya matumizi ya takwimu zinazotolewa katika ripoti ya TEITI na wananchi watafahamu malipo na kodi zinazolipwa na Kampuni Serikalini, gharama za uwekezaji na uzalishaji katika sekta hizo.

Pamoja na mambo mengine, Dkt. Biteko amesema ripoti inayotolewa na TEITI ni nyaraka na nyenzo muhimu kwani zinaweka wazi takwimu mbalimbali kuhusu taarifa za tozo nyingine zinazolipwa Serikalini na Kampuni za rasilimali hizo.

Amesema, hadi sasa TEITI imeshakamilisha na kuweka wazi ripoti 12 zenye takwimu za malipo ya Kampuni za Madini na Gesi Asilia kwa kipindi cha Julai 1, 2008 hadi Juni 30, 2020 ambapo zimebainisha kuwa, Serikali imekusanya kiasi cha dola za Marekani bilioni 4.30 kutoka Kampuni za Madini, Mafuta na Gesi Asilia.

Naye, Mkuu wa Mkoa wa Songwe Waziri Kindamba ameipongeza Wizara ya Madini kwa kuona umuhimu wa kutoa elimu hiyo kwa Jamii mkoani humo na kuwataka washiriki kuwa mabalozi wazuri baada ya kupata elimu kupitia mafunzo hayo ili kuleta uelewa zaidi kwa jamii yao kuhusu majukumu ya TEITI hususan suala la uwazi na uwajibikaji.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Mkwajuni Saibati Kapingu ameipongeza TEITI kwa kutoa elimu juu ya majukumu ya taasisi hiyo ambapo ameonesha kuelewa na kuahidi kufuatilia miradi, kuwasilisha taarifa katika Halmashauri na kuhimiza uwajibikaji na kuiomba TEITI iendele kutoa elimu kama hizo pale watakapoweza kufika kwa kuwezesha wananchi kufahamu mapato na kodi zitokanazo na sekta ya uziduaji.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages