Breaking

Sunday 7 January 2024

WAZIRI JAFO AWEKA JIWE LA MSINGI UJENZI WA HOTELI ZANZIBAR

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt Selemani Jafo amesema Wananchi wa Zanzibar wanastahili kujivunia maendeleo yaliyopatikana kwa muda mfupi.

Amesema hayo wakati akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa Hoteli ya Kiwengwa Tembo Beach iliyopo Mkoa wa Kaskazini Unguja ikiwa ni shamrashamra za Maadhimisho ya Miaka 60 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.

Waziri Dkt. Jafo ameeleza kuwa uwekezaji wa miradi ikiwemo afya, elimu, miundombinu na uwanja wa ndege unaofanyika chini ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) ya Awamu ya Nane ni fursa kubwa kwa wananchi kwani inawaletea kipato pamoja na kukuza uchumi.

Amesema viongozi hao wakuu wa Serikali hizo mbili pia wameonesha dhamira ya kuifanya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa na mapinduzi ya viwanda ambavyo vimekuwa ni sehemu ya uwekezaji na hivyo kukuza uchumi.

Dkt. Jafo amefafanua kuwa viongozi wamefungua milango ya uwekezaji mkubwa wa ndani na nje ya nchi kwa kujenga na kuimarisha miundombinu muhimu, itakayoweza kutoa fursa za kimaendeleo kwa Wananchi.

Pamoja na hayo, Waziri Dkt. Jafo ametoa wito kwa wawekezaji kote nchini kuzingatia uhifadhi wa mazingira katika maeneo yao ili kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi zinazoikabili dunia.

Amesema kuwa athari za mabadiliko ya tabianchi zinaweza kuathiri kwa kiasi kikubwa sekta zinazoingiza mapato hasa utalii, kwa hiyo ni wajibu wa kila mmoja kushiriki kikamilifu katika shughuli za kuhifadhi mazingira zikiwemo kupanda miti.

Vilevile, Dkt. Jafo ametoa wito kwa wananchi kutunza na kusafisha fukwe zilizopo katika maeneo mbalimbali ili ziwe katika mazingira safi na ya kuvutia ikiwa ni sehemu ya kukuza uchumi wa buluu kama ambavyo unachagizwa na Serikali.
Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt Selemani Jafo akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa Hoteli ya Kiwengwa Tembo Beach iliyopo Mkoa wa Kaskazini Unguja ikiwa ni shamrashamra za Maadhimisho ya Miaka 60 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.
Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt Selemani Jafo akizungumza wakati wa hafla ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa Hoteli ya Kiwengwa Tembo Beach iliyopo Mkoa wa Kaskazini Unguja ikiwa ni shamrashamra za Maadhimisho ya Miaka 60 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.
Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt Selemani Jafo akizungumza na mwekezaji Hussein Muzamil wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa Hoteli ya Kiwengwa Tembo Beach iliyopo Mkoa wa Kaskazini Unguja ikiwa ni shamrashamra za Maadhimisho ya Miaka 60 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar. Kulia ni Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Khamis Hamza Khamis na Mkurugenzi wa Mamlaka ya Kukuza Uwekezaji Zanzibar (ZIPA) Bw. Shariff Ali Shariff.
Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt Selemani Jafo akikagua maendeleo ya ujenzi wa Hoteli ya Kiwengwa Tembo Beach iliyopo Mkoa wa Kaskazini Unguja ikiwa ni shamrashamra za Maadhimisho ya Miaka 60 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar. Kulia kwa Waziri ni Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja Mhe. Rashid Hadid Rashid na mbele ni Mkurugenzi wa Mamlaka ya Kukuza Uwekezaji Zanzibar (ZIPA) Bw. Shariff Ali Shariff.

Waziri wa nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt Selemani Jafo akiwa katika picha ya pamoja na viongozi mbalimbali wakati wa hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa Hoteli ya Kiwengwa Tembo Beach iliyopo Mkoa wa Kaskazini Unguja ikiwa ni shamrashamra za Maadhimisho ya Miaka 60 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages