Breaking

Wednesday 8 June 2022

AJALI NYINGINE YA TRENI YAUA WATU 17 NA KUJERUHI 50 - IRAN

Na Said Muhibu, Lango La Habari 


Watu 17 wamefariki dunia na wengine 50 kujeruhiwa katika ajali ya treni iliyotokea jijini Tabas nchini Iran alfajiri ya leo Juni 08, 2022.


Treni hiyo, iliyokuwa imebeba abiria 348, ilitoka kwenye mstari kati ya miji ya Mashhad na Yazd takriban kilomita 50 (maili 31) kutoka Tabas.


Kwa mujibu wa televisheni ya taifa ya Iran mabehewa manne kati ya saba yaliacha njia karibu na jiji la jangwa la Tabas na kuanguka huku ripoti za awali zikisema chanzo cha ajali ni kutokana na treni hiyo kugongwa na mchimbaji aliyekuwa karibu na njia ya reli ambapo afisa mmoja alisema huenda ikawa mchimbaji huyo alikuwa akiendeleza ukarabati wa mradi wa ujenzi wa reli hiyo.

Vikosi vya uokoaji vilivyo na magari ya kubebea wagonjwa na helikopta vimewasili katika eneo husika huku takriban watu 16 wamepata majeraha mabaya, na wengine kuhamishiwa hospitali za mitaa.

Gavana wa Kaunti ya Tabas Ali Akbar Rahimi aliambia vyombo vya habari vya serikali kuwa mabehewa manne kati ya saba ya treni hiyo yaliangushwa kwenye njia.


Iran ambayo tayari inakabiliwa na vikwazo vya nchi Marekani kutokana na kuvunjika kwa mkataba wake wa nyuklia, imekuwa ikiomboleza vifo vinavyotokana na ajali mbalimbali za treni huku maafa makubwa zaidi ya treni nchini Iran yakitokea mwaka 2004 wakati treni iliyokimbia iliyokuwa na petroli, mbolea, salfa na pamba ilipoanguka karibu na mji wa kihistoria wa Neyshabur, na kuua takriban watu 320, kujeruhi wengine 460 na kuharibu vijiji vitano.

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages