Breaking

Wednesday 13 July 2022

NAIBU WAZIRI MASANJA AHAMASISHA WANANCHI KUJITOKEZA KUHESABIWA ZOEZI LA SENSA




Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Mwanza, Mhe. Mary Masanja amewataka wananchi kujitokeza kuhesabiwa katika zoezi la Sensa ya Watu na Makazi linalotarajiwa kufanyika Agosti 23, 2022.

Ametoa kauli hiyo leo Jumatano Julai 13, 2022 alipokuwa akizungumza katika kikao cha wajumbe wa Baraza la Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Wilayani Magu.

“Tunaenda kwenye Sensa tarehe 23 Agosti 2022 hivyo kila mmoja wetu ajiandae kuhesabiwa” Mhe. Masanja amesisitiza.



Amesema lengo la Sensa ni kuisaidia Serikali kutambua idadi ya wananchi walio katika maeneo wanayoishi ili kupata idadi kamili ya watanzania wote ili huduma zinazotolewa zilingane na idadi ya wananchi ikiwemo huduma za afya, elimu, maji , barabara na huduma nyinginezo za kijamii.

Aidha, amewataka viongozi wa Jumuiya ya Wanawake, viongozi wa Kata na kila Wilaya kuendelea kuhamasisha wananchi kujitokeza kuhesabiwa kila wanaposimama katika majukwaa.

Katika hatua nyingine, Mhe. Masanja amewataka wanajumuiya wa UWT Magu kushirikiana katika utekelezaji wa majukumu mbalimbali hasa katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi wa viongozi.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages