Breaking

Thursday 22 September 2022

WAFANYABIASHARA WA MKAA WATAKIWA KUFUATA SHERIA, KANUNI NA TARATIBU



Serikali imewataka wananchi wanaofanya biashara ya mkaa kufuata Sheria, Kanuni na Taratibu kwa kuwa kumekuwepo na wimbi la uvunaji wa mazao ya misitu, ukataji na uchomaji wa mkaa bila kufuata sheria, kanuni na taratibu zinazosimamia biashara hiyo.

Hayo yamesemwa leo Septemba 22,2022 na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii alipokuwa akijibu swali la Nicodemus Maganga (Mbogwe).

“Inapotokea mwananchi anasafirisha mazao ya misitu (mkaa) bila kufuata utaratibu, mazao hayo hutaifishwa na Serikali” Mhe. Masanja amesisitiza.

Amesema uvunaji holela wa mkaa umesababisha kutoweka kwa kasi kwa maeneo ya misitu na hatimaye kujitokeza kwa athari za mabadiliko ya tabia nchi.

Kuhusu kauli ya Serikali juu ya askari wa Misitu wanaopiga na kuwanyang’anya mkaa wananchi wa Mbogwe, Mhe. Masanja amesema 

Wizara haitosita kuwachukulia hatua watumishi wake wanaohusika na uvunjaji huo wa sheria, kanuni na taratibu.

Pia, amewataka Wananchi kutoa taarifa kwa vyombo vya ulinzi na usalama wanapotendewa vibaya na watumishi hão ili hatua stahiki zichukuliwe.

Akijibu swali la Mbunge wa Tabora Mjini, Emmanuel Mwakasaka kuhusu lini Serikali itatoa vibali vya Uwindaji, amesema Vibali vya uwindaji wa kitalii vinaendelea kutolewa kwa mujibu wa Kanuni husika ambapo hadi sasa jumla ya minada saba (7) imefanyika na wadau wamepewa vibali vyao.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages