Breaking

Friday 23 September 2022

SERIKALI KUENDELEA KUVITANGAZA NA KUVIENDELEZA VIVUTIO VYA UTALII UKEREWE, KITULO



Serikali imeendelea kuvitangaza na kuviendeleza vivutio mbalimbali vya utalii kwa kushirikiana na wadau wa utalii nchini.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii alipokuwa akijibu maswali kuhusu uendelezaji wa vivutio vya utalii vya Wilayani Ukerewe na uboreshaji wa Hifadhi ya Taifa Kitulo Bungeni jijini Dodoma leo.

Amesema katika Kisiwa cha Ukerewe Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kushirikiana na Maafisa wa Mkoa wa Mwanza walitekeleza zoezi la kubaini na kuvitambua vivutio vya utalii vilivyopo katika kisiwa hicho.

“Vivutio vilivyotambuliwa ni pamoja na utalii wa ikolojia, utalii wa fukwe, utalii wa kiutamaduni na kihistoria” Mhe. Masanja amefafanua.

Amesema ili kuboresha utalii wa êneo hilo Serikali inaendelea kuimarisha Ofisi ya Kanda ya Utalii iliyopo Jijini Mwanza na kuanzisha Chuo cha Utalii cha Taifa katika Mkoa wa Mwanza kwa lengo la kusogeza huduma Kanda ya Ziwa.

Aidha, amesema Wizara imeendelea kuboresha miundombinu ya barabara ndani ya Hifadhi ya Taifa Kitulo, kuanzisha huduma za malazi na chakula, kuongeza mazao mapya ya utalii kama vile utalii wa kutumia baiskeli, utalii wa kutembea kwa miguu na utalii wa kupanda vilima.

Ameongeza kuwa Serikali inaendelea kutangaza fursa za uwekezaji zilizopo ndani ya Hifadhi hiyo ili kuongeza idadi ya watalii na idadi ya siku za kukaa hifadhini na hivyo kuongeza mapato.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages