Breaking

Saturday 15 October 2022

RAIS SAMIA ATOA MAAGIZO KWA WIZARA YA MADINI



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan ameipongeza Wizara ya Madini kwa kuendelea kufanya vizuri katika kuisimamia Sekta hiyo hapa nchini ili iwe chachu ya kitovu cha uchumi.

Akizungumza na wananchi wa Mkoa wa Geita katika uwanja wa shule ya msingi Kalangalala Rais Samia amesema Wizara ya Madini inafanya vizuri katika usimamizi wa Sekta hiyo lakini inapaswa kuongeza bidii hususan katika kutoa elimu ya Sheria na Kanuni za madini kwa wachimbaji.

Aidha, amesema kuwa Serikali inatambua mchango wa wananchi wa mkoa wa Geita katika ujenzi wa uchumi hususan kwa kupitia shughuli za uchimbaji wa madini.

"Ni kweli kabisa kiwango kikubwa cha madini ya dhahabu kinapatikana hapa Geita na inachimbwa ndani ya mkoa wa Geita, mchango wa mkoa wa Geita ni zaidi ya asilimia 50 ya dhahabu yote inayochimbwa Tanzania," amesema Rais Samia.

Mara baada ya kuzindua kiwanda cha kusafisha dhahabu, Rais Samia amewataka wanachi wa Geita na mikoa yote inayochimba madini ya dhahabu kuvitumia viwanda vya kisasa vya kusafisha na kuchenjua dhahabu vilivyopo nchini mara baada ya kuzindua kiwanda cha Mama Masasi cha Geita.

"Niombe sana tupeleke dhahabu zetu huko zikachenjuliwe ili Tanzania iongeze thamani ya madini ya dhahabu yenye thamani kubwa," amesisitiza.

Vile vile, ameiagiza Wizara ya Madini kufanya ukaguzi wa mara kwa mara ili kuhakikisha shughuli za utafiti, uchimbaji, uchenjuaji na biashara za madini zinafanywa kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Miongozo inayosimamia Sekta ya Madini.

Vile vile, Rais ameitaka wizara kuendelea kutoa elimu juu ya Sheria ya Madini na Kanuni zake kwa wadau mbalimbali kupitia mafunzo maalum.

Rais Samia ameitaka Wizara ya Madini kuendelea kushirikiana na idara nyingine za Serikali na vyombo vya Dola mkoani na katika sehemu nyingine ambayo kuna uchimbaji mkubwa katika kusimamia shughuli za uzalishaji na biashara ya madini na kudhibiti vitendo vya utoroshaji wa madini.

Pia, ameagiza wizara kuendelea kuwaunganisha wachimbaji wadogo na Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) kwa lengo la kupata taarifa za kijiolojia yenye madini, elimu ya masuala ya utafiti, uchimbaji na uchenjuaji ili kuongeza tija kwenye shughuli zao.

Kuhusu suala la kodi kwa wachimbaji ameiagiza Wizara ya Madini kukutana na Wizara ya Fedha kuziangalia na kuwasikiliza wadau na wafanyabiashara kuhusu kodi zinazoleta kero na kupunguza kasi ya utendaji kwa wawekezaji wanaowekeza katika Sekta hiyo.

Naye, Waziri wa Madini Dkt. Doto Biteko amesema, mkoa wa Geita ni mkoa kinara wa dhahabu nchini. Ameongeza Geita ni ya kwanza katika mikoa inayozalisha dhahabu hapa Tanzania.

Dkt. Biteko amemhakikishia Rais Samia kuwa Sekta ya Madini itafikia lengo la makusanyo iliyopangiwa kupitia miradi mbalimbali ya uchimbaji madini inayoendela sasa katika maeneo mbalimbali.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages