Breaking

Monday 12 December 2022

WAZIRI DKT. GWAJIMA ATAKA MIONGOZO YA MAENDELEO NA USTAWI IWAFIKIE WANANCHI



Na WMJJWM, Mafia

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanwake na Ma kundi Maalum Mhe. Dkt Dorothy Gwajima, amewaagiza Maafisa Maendeleo na Ustawi wa Jamii nchini kuhakikisha wananchi wanaifahamu miongozo inayohusu maendeleo na Ustawi wa Jamii.

Waziri Dkt Gwajima ametoa agizo hilo wakati akishiriki na kujibu maswali ya wananchi waliotaka kufahamu aina za mikopo ya uwezeshaji wanawake kiuchumi na taratibu za kufuata, katika Kongamano la Wanawake wa Halmashauri ya Wilaya ya Mafia, Wilayani Mafia, mkoa wa Pwani Desemba 11, 2022.

Ameitaja miongozo hiyo kuwa ni pamoja na mwongozo wa uundaji na uendeshaji majukwaa ya uwezeshaji wanawake kiuchumi, mwongozo wa mkopo wa asilimia kumi na mkopo wa WDF na mingine ya uwezeshaji wananchi kiuchumi kwa ujumla wake.

"Ninasikitika kuona kuwa wananchi hadi leo hawafahamu aina za mikopo hiyo na taratibu zake ilihali miongozo tulitoa na ilielimishwa kwenye kikao cha Maafisa Maendeleo ya Jamii wote walipokuja Jijini Dodoma kutoka mikoa na Halmashauri zote nchini Tanzania hivyo, naelekeza ufahamishaji viongozi na wananchi kuhusu miongozo hii na mingine yote ufanyike kwani nitakuwa nafuatilia kwa wananchi moja kwa moja" amesema Waziri Gwajima

Aidha, Waziri Gwajima ameendelea kusisitiza suala la usambazaji wa miongozo hiyo kufanyika kwa gharama nafuu kwa msaada wa teknolojia ya kidigitali ambapo, wananchi wenye uwezo wa kutumia teknolojia hiyo watafahamishwa na wasio na uwezo watapata kupitia ofisi za vijiji, kata na jumuiya za kijamii.

Amesema bila kufanya hivyo, kuna hatari juhudi za Serikali kuishia kwenye ufahamu wa watu wachache huku kundi kubwa la watanzania wenye uhitaji wa kujiendeleza likiachwa nyuma jambo ambalo siyo nia ya Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyeanzisha Wizara ya Maendeleo ya Jamii.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Mafia Mhe. Injinia Martin Ntamo ameahidi kusimamia kuhakikisha maelekezo hayo yanatekelezwa kuhakikisha wadau wote wamepatiwa.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mafia Kassim Ndumbo ameahidi kutekeleza maelekezo hayo ambapo ilielezwa kuwa utaratibu wa kusambaza miongozo hiyo umeshaanza.

Kongamano hilo lillikuwa ni kuhitimisha kampeni ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia ambapo lilibebwa na kaulimbiu ya Wezesha Mwanamke wa Mafia Kiuchumi; Tokomeza Ukatili wa Kijinsia.

MWISHO
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages