Breaking

Sunday 22 January 2023

MCHENGERWA ATATUA MGOGORO BAINA YA MWEKEZAJI NA WANANCHI RUFIJI



Na John Mapepele

Wananchi wa eneo la Nyanda na Utunge wilayani Rufiji wamemshukuru Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mbunge wa Rufiji na MNEC wa Mkoa wa Pwani, Mhe. Mohamed Mchengerwa kwa kutatua mgogoro wa muda mrefu baina ya mwekezaji wa mradi wa uzalishaji wa sukari na wananchi wa maeneo hayo.

Akizungumza mara baada ya kumalizika kwa mkutano wa wananchi na Mhe. Mchengerwa leo, Januari 22,2023 kwenye eneo la Nyanda, Mwenyekiti Mstaafu wa Kijiji hicho, Amir Omary Magulu amempongeza Mhe. Mchengerwa kwa busara na jitihada zake za kuumaliza mgogoro huo ambao ulikuwa sugu kwa muda mrefu sasa.

Amesema mgogoro huo baina ya mwekezaji huyo ambaye ni Lake Agro unatokana na ukiukwaji wa makubaliano ya awali ya kupewa eneo la uwekezaji na kutopata taarifa sahihi za uwekezaji.

Akitoa suluhisho la mgogoro hilo, Mhe. Mchengerwa ameuomba uongozi wa Wilaya na Halmashauri ya Rufiji kuja kwa wananchi pamoja na mwekezaji ili kujadili kwa uwazi uwekezaji huo ili kurekebisha tofauti hizo na kuendelea kutekeleza mradi huo mkubwa wa pili nchini wa uzalishaji wa sukari.


Amefafanua kuwa changamoto iliyopo ni mawasiliano hafifu ya mwekezaji kwa wananchi ambayo yamesababisha wananchi kutoelewa kinachoendelea katika mradi huo.

Ameongeza kuwa, uongozi wa Wilaya na Halmashauri usimamie makubaliano yaliyofikiwa awali na kwamba mwekezaji asipewe eneo la pili alilolitaka hadi akae na kukubaliliana na wananchi wa maeneo hayo.

Aidha, amesema Serikali inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan tayari imeshatoa fedha nyingi kwa ajili ya kusaidia wananchi wa Tanzania ikiwa ni pamoja na wanarufiji ambapo amesema kwa upande wa Rufiji tayari Serikali imetenga Bilioni 46 kujenga barabara ya Nyamwage hadi Utete pia kutoka Ikwiriri hadi Mkongo.

Kwa upande wao, Rashidi Omari Goboleni na Asha Juma Mbonde wamemshukuru na kumpongeza Mhe. Mchengerwa kwa maelekezo yake ya kumaliza mgogoro huo huku wakisifu jitihada mbalimbali zinazofanywa na Serikaliza kuwaletea maendeleo.

“Tumefurahishwa sana na ujio wa Mbunge wetu leo na kumaliza kabisa mgogoro huu, natumaini sasa tutapiga hatua. Asante sana mama Samia kwa kutushika mkono” ameongeza Nyamkiu Mohamed Mkiu mkazi wa Kijiji cha Utunge


Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages