Breaking

Saturday 28 January 2023

WATU 165 WAKAMATWA KWA TUHUMA ZA WIZI, UBAKAJI NA MAUAJI



Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limefanikiwa kuwakamata watuhumiwa 165 wakiwemo wa makosa ya wizi, ubakaji, mauaji na kukutwa na bidhaa za magendo na pombe haramu.

Akitoa taarifa ya mafanikio ya mwezi mmoja mbele ya waandishi wa habari Januari 27, 2023 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Kamishna Msaidizi wa Polisi ACP Benjamin E.Kuzaga amesema watuhumiwa hao waliokamatwa wamo wanaofanya wizi kwa njia ya Mtandao, kupatikana na nishati ya mafuta isivyo halali, kubaka, wizi wa pikipiki, Kupatikana na bidhaa za magendo, Kupatikana na pombe ya moshi na kupatikana na kiwanda bubu cha kutengeneza pombe kali.

Kamanda Kuzaga amesema misako hiyo imepatikana Pombe haramu ya moshi (Gongo) ujazo wa lita 366. mitambo miwili ya kutengenezea Gongo na pikipiki 04 mali za wizi zilikamatwa, mali ya wizi vitenge doti 38 vikisafirishwa kwenye gari T. 948 ASL Toyota Mark X rangi ya nyeupe zilikamatwa.

Ameongeza kuwa, katika misako hiyo watuhumiwa wa matukio ya Mauaji 19 kati yao wanaume 16 na wanawake 03 akiwemo mama aliyemuua mtoto wake huko Wilaya ya Rungwe kwa tuhuma za wizi wa fedha wamekamatwa.

Aidha Kamanda Kuzaga ametoa wito kwa wananchi kuacha kujihusisha na vitendo vya kihalifu badala yake kufanya kazi halali za kujipatia kipato. Aidha, ametoa wito kwa wazazi kuongeza umakini katika ulinzi na malezi ya watoto ili kuwaepusha na vitendo vya kikatili kama vile ubakaji, ulawiti na vingine.

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages