Breaking

Tuesday 17 January 2023

WAZIRI MCHENGERWA ATOA MAELEKEZO MAZITO KWA KAMATI YA MDUNDO WA TAIFA



Na John Mapepele

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Mohamed Mchengerwa leo amekagua maendeleo ya Kamati ya Kutafuta Mdundo wa Taifa na kuipongeza kwa hatua iliyofikia huku akiitaka kukamilisha kazi hiyo mara moja ili mdundo wa Tanzania uteke soko la Afrika na Dunia kwa ujumla.

Mhe. Mchengerwa amesema dhamira ya Serikali ni kufanya uwekezaji mkubwa kwa wasanii wengi wa Tanzania ili wafike kwenye ngazi ya kimataifa kama mataifa mengine yanayofanya vizuri duniani.



Ameiagiza Kamati hiyo inayosimamiwa na Mtendaji Mkuu wa Baraza la Sanaa la Taifa ( BASATA) Dkt. Kedmon Mapana kuainisha wasanii kumi watakaosaidiwa na Serikali ambao wanatumia midundo hiyo kuandaa miziki itakayotambulisha mdundo huo

Aidha, ameitaka Kamati kuandaa mkakati wa kuutangaza ( kupromote) mdundo huo wa taifa ili ukubalike na ujulikane duniani



Ameelekeza nyimbo hizo zirekodiwe pia kwenye video ili kupeleka ujumbe mahususi uliokusudiwa.

Mhe. Mchengerwa ameelekeza pia kuwa siku ya uzinduzi rasmi wa mdundo wa taifa nyimbo hizo ziwe zimerekodiwa na kutumbuizwa mubashara katika mitandao mbalimbali duniani.



Kwa upande wake mjumbe wa Kamati hiyo zahir Ally Zolo amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kufanya uwekezaji mkubwa kwenye sekta za sanaa.

Amesema, Mhe. Rais amefanya mapinduzi makubwa katika kipindi kifupi cha utawala wake.

Amempongeza waziri Mchengerwa kwa usimamizi madhubuti wa Wizara yake ambao amedai umeleta mafanikio makubwa.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages