Breaking

Thursday 9 February 2023

MCHENGERWA AWATAKA MADIWANI KUTANGULIZA MBELE MASLAHI YA WANANCHI




Na John Mapepele

Waziri wa Utamaduni Sanaa na Michezo, MNEC wa Mkoa wa Pwani na Mbunge wa Rufiji, Mhe. Mohamed Mchengerwa amewataka madiwani wa Rufiji kutanguliza mbele maslahi ya Wananchi wakati wote wa maamuzi ili kuwaletea wananchi maendeleo.

Mhe. Mchengerwa ameyasema haya Februari 8, 2023 kwenye mkutano maalum wa Baraza la madiwani wa Rufiji kujadili Taarifa ya Ugawaji wa Ardhi ya Rufiji kwa wawekezaji waliojitokeza kuwekeza.

" Niwaombe sana tutangulize maslahi ya wananchi wa Rufiji kama miradi tunakwenda nao tunasema utatuwezesha kuwapatia ajira wananchi wetu zaidi ya elfu kumi hatuna sababu ya kumkataa mwekezaji" amefafanua Mhe. Mchengerwa wakati alipokuwa akizungumzia miradi wa uzalishaji wa sukari.


Mradi huu wa uzalishaji wa sukari unafanywa na mwekezaji Lake Group ni mradi wa pili kwa ukubwa hapa nchini kwa uzalishaji wa sukari ukiondoa ule unatekelezwa wilayani Bagamoyo.

Aidha, amewapongeza madiwani hao kwa kuhamasika na kuhoji uwekezaji inayofanyika huku akiwasisitiza kuendelea kuhoji mambo ya maendeleo ya wananchi kwa maslahi mapana ya wananchi kwani kwa kufanya hivyo ni haki yao ya msingi ya kupata taarifa.


Ameongeza kuwa kuhoji na kufahamu vizuri miradi mbalimbali inayofanyika katika kipindi hiki kutawafanya wawe mabalozi wazuri wa kuisemea Serikali maendeleo makubwa yanayofanyika huku akipongeza Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa aliyokwisha ifanya ya kuwaletea maendeleo wanarufiji na watanzania kwa ujumla katika kipindi hiki kifupi.

Katika siku za hivi karibuni, Mhe. Mchengerwa alifanya mkutano wa hadhara na wananchi wa vijiji vyote vinavyoguswa na mradi huo na kujadiliana nao ambapo walikubaliana na mradi huo kwa kauli moja huku wakitaka mwekezaji kuja kujadiliana nao badala ya kuwa na uwakilishi wakati wa vikao miongoni mwao.


Walimshukuru Mhe. Rais kupitia kwa Mbunge wao kwa mapinduzi makubwa ya kuwaletea huduma za jamii na kuwajengea miundombinu hususan barabara za lami katika jimbo la Rufiji.

Wakati huohuo Kaimu Mwenyekiti wa Baraza hilo, Mhe. Ally Ndungutu amemshukuru Mbunge wa Rufiji, Mhe. Mchengerwa kwa kumaliza mgogoro huo baada ya kuamua kuja kwa wananchi wanaozunguka katika mradi huo na kuwasiliza kero zao.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages