Breaking

Monday 20 February 2023

SERIKALI YAJA MWONGOZO WA UPANGAJI MAKAZI NA UJENZI WA NYUMBA VIJIJINI



Na Munir Shemweta, WANMM MBEYA

Ili kuondokana na changamoto za upangaji vijijini, Serikali kupitia Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeandaa wa mwongozo wa upangaji makazi na ujenzi wa nyumba vijijini.


Ingawa upangaji wa vijiji na ujenzi wa nyumba bora vijijni unapaswa kuhusisha watu wote, serikali imeona ni vyema kutoa muongozo kwa kutumia lugha rahisi inayoeleweka kuelezea kanuni muhimu za kuzingatiwa na mamlaka na wana kijiji katika kupanga makazi ya vijiji bila kutegemea kutoka kwa wataalamu.


Hayo yamebainishwa na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula leo tarehe 20 Februari 2023 katika kikao kazi cha kujadili na kuweka mikakati wa kukwamua zoezi la urasimishaji makazi kilichofanyika mkoani Mbeya.


Kwa mujibu wa Dkt Mabula, miongozo iliyozingatiwa katika uandaaji mwongozo huo ni pamoja na uandaaji wa mipangokina ya makazi vijijini pamoja na mwongozo wa utoaji vibali vya ujenzi na usimamizi wa ujenzi wa majengo kwenye mamlaka za serikali za mitaa wa mwaka 2018.


Alisema, eneo la Makazi la kijiji ni sehemu ya mpango wa jumla wa Matumizi ya Ardhi ya kijiji unaoainisha maeneo kwa ajili ya matumizi mbalimbali kama vile makazi, biashara, taasisi, kilimo , misitu , malisho ya mifugo na huduma za jamii na miundombinu.


Alibainisha kuwa, pamoja na kuainishwa kwa matumizi mbalimbali kwenye vijiji lakini maeneo hayo kwa muda mrefu yamekuwa hayapatiwi umuhimu na mamlaka za upangaji katika kuzijengea uwezo serikali za vijiji ili kuyaandalia mipango kina ya kusimamia ukuaji wake kama miji ya baadaye.


‘’vitovu vya vijiji vinapaswa kupangwa ili kuwezesha jamii kuishi kwa njia ya usawa na kufanya shughuli zao katika mazingira bora na kuweza kutoa fursa za kutosha za ajira na mandhari mazuri ya kuvutia na kuchangia katika maendeleo ya ukuaji uchumi’’ alisema Dkt Mabula.


Hata hivyo, Dkt Mabula alisema kutokana na mwenendo huo bado kuna jukumu kubwa la kupanga matumizi ya ardhi ya vitovu vya vijiji na hususana makazi ili kupunguza migogoro na kuhakikisha kwamba vijiji vinakuwa na milki salama , mazingira bora ya makazi na muunganiko wa shughuli nyingine za kiuchumi kama vile kilimo, ufugaji, uvuvi na hifadhi ya mazingira.


Kwa upande wake Kamishna wa Ardhi nchini Nathaniel Methew Nhonge amesema, kwa muda sasa kumekuwa na majengo kutopangwa na hivyo kushindwa kuakisi taswira nzuri ya uendelezaji miji nchini.


Kwa mujibu wa Nhonge, makazi holela nchini yanachangiwa kwa kiasi kikubwa na maeneo ya kutoka mamlaka za udhibiti kutofanya vizuri pamoja na kiasi cha fedha kinachotengwa kwa shughuli za upangaji.


‘’Eneo lingine ni kutotengwa fedha za kutosha ili kutekeleza miradi ya kupanga, kupima na kumilikisha ardhi suala alilolieleza linachangia miji holela na jambo hilo limesababisha wizara kuja na program ya urasimishaji makazi’’ alisema Nhonge.


Kikao kazi cha siku moja kujadili na kuweka mikakati wa kukwamua zoezi la urasimishaji makazi holela katika mkoa wa Mbeya kinahusisha viongozi mbalimbali wakiwemo wakuu wa wilaya, wakurugenzi wa halmashauri, madiwani, wataalamu wa sekta ya ardhi pamoja na makampuni yayofanya kazi za urasimishaji makazi holela.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages