Breaking

Sunday 24 September 2023

RUZUKU KUTOKA REA YAWEZESHA UTEKELEZAJI MRADI WA UMEME KILOLO

Na Mwandishi Wetu, Iringa

WAKALA wa Nishati Vijijini (REA) umesema utahakikisha unashirikiana na
sekta binafsi katika kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora na nishati
ya uhakika vijijini.

Mkurugenzi waTeknolojia za Nishati Jadidifu na Nishati Mbadala wa REA, Mhandisi Advera Mwijage alisema hayo baada ya kukagua maendeleo ya mradi wa ujenzi wa
umeme wa maji (kilovoti 2400) wa Idete wilayani Kilolo unaotekelezwa na Kampuni ya Lung’ali Natural Resources Co ltd.

Amesema REA mpaka sasa imeishatoa ruzuku ya shilingi bilioni 4 kwa mradi huo
ulio chini ya Kanisa Katoliki mkoani Iringa ambazo zimetumika kwa
utafiti wa mazingira, ujenzi wa bomba la maji na jengo lenye mtambo wa kuzalishia umeme (Power House).

Pia, amesema REA ina wajibu wa kuwaunganisha wazalishaji wadogo na
taasisi zinazotoa mikopo kwa riba nafuu ambapo Benki ya TIB imeikopesha
kampuni hiyo ili ikamilishe mradi huo wa umeme kwa wakati na kuingiza kwenye gridi
ya taifa.

“REA inafanya kazi na sekta binafsi katika kuhakikisha
upatikanaji wa huduma bora ya nishati vijijini na kuchangia katika
shughuli za uchumi zinazoongeza kipato kwa wananchi,” alisema Mhandisi Mwijage.

Aliongeza kuwa serikali peke yake haiwezi kufanya kila kitu hasa
katika miradi ya maendeleo inayogusa wananchi na hivyo kutambua
umuhimu wa ushiriki wa sekta binafsi.

Serikali imekuwa ikiipatia REA fedha ili kuwawezesha kufadhili miradi
ya wazalishaji wadogo binafsi wa umeme ili miradi hiyo ichangie katika kiasi cha umeme
kinachozalishwa katika gridi ya taifa .

Mhandisi Mwijage ameweka wazi umuhimu wa wazalishaji wadogo wa umeme, katika
maendeleo ya wananchi, na kusema serikali itaendelea kushirikiana nao.

Akieleza zaidi, amesema kuwa miradi ya uzalishaji umeme wa maji inasaidia kupunguza uzalishaji wa hewa ya ukaa na inatunza mazingira hasa kwa kuwezesha kuachana na matumizi ya jenerata katika kuzalisha umeme.

“Miradi hii pia inaiongezea serikali kipato kwa kulipa kodi, kuzalisha
ajira na kuwapa wananchi uhakika wa upatikanaji wa umeme na hivyo
kushiriki kikamilifu katika shughuli za kujiongezea kipato,” alisema
Mkurugenzi wa Nishati Mbadala na Teknolojia.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni inayozalisha umeme huo wa
maji, Lung’ali Natural Resources, Padre Luciano Mpoma alisema
wanatarajia kuanza uzalishaji wa umeme Januari mwakani na kwamba ujenzi
unaendelea vizuri.

Mradi huo utakapokamilika amesema wananchi wa Idete na maeneo mengine
watakuwa na umeme wa uhakika na hivyo kuweza kushiriki kikamilifu
katika shughuli za kiuchumi na huduma za kijamii.

Naye Mwenyekiti wa Kata ya Kidete, Henry Kikoti ameelezea shauku ya
wananchi kutaka mradi huo ukamilike kwani utaenda kuwa suluhu kwa
umeme wa uhakika kwani uliopo hautoshelezi mahitaji ya shughuli za
kiuchumi hasa kutokana na maendeleo na uwekezaji wa wananchi katika
nyanja mbalimbali za kiuchumi.
Mkurugenzi wa Teknolojia za Nishati Jadidifu na Nishati Mbadala kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Advera Mwijage, akikagua maendeleo ya ujenzi wa Mradi wa ujenzi wa umeme wa maji (kilovoti 2400) wa Idete wilayani Kilolo unaotekelezwa na Kampuni ya Lung’ali Natural Resources Co Ltd, Septemba 23, 2023. Wakala wa Nishati Vijijini (REA) unafadhili Mradi huu ili kuwezesha kuongeza umeme katika gridi ya taifa.
Kazi ya ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme urefu wa mita 641 ikiendelea Septemba 23, 2023 katika eneo la Mradi wa Kuzalisha umeme wa maji (kilovoti 2,400) Idete wilayani Kilolo, Mkoa wa Iringa, unaotekelezwa na Kampuni ya Lung’ali Natural Resources Co. Ltd. Wakala wa Nishati Vijijini (REA) unafadhili Mradi huu ili kuwezesha kuongeza umeme katika gridi ya taifa.
Taswira ya Bwawa la kuhifadhia maji ya kuzalisha umeme pamoja na mtandao wa mabomba ya kusafirishia maji kupeleka kwenye mtambo wa uzalishaji umeme katika eneo la Mradi wa kuzalisha umeme wa maji (kilovoti 2,400) Idete wilayani Kilolo, Mkoa wa Iringa, unaotekelezwa na Kampuni ya Lung’ali Natural Resources Co. Ltd. Wakala wa Nishati Vijijini (REA) unafadhili Mradi huu ili kuwezesha kuongeza umeme katika gridi ya taifa. Taswira hii ilichukuliwa Septemba 23, 2023 wakati wa ziara ya Mkurugenzi wa Teknolojia za Nishati Jadidifu na Nishati Mbadala kutoka REA, Mhandisi Advera Mwijage.
Taswira ya Mtandao wa Bomba la kusafirishia maji kupeleka kwenye Mtambo wa uzalishaji umeme katika eneo la Mradi wa kuzalisha umeme wa maji (kilovoti 2,400) Idete wilayani Kilolo, Mkoa wa Iringa, unaotekelezwa na Kampuni ya Lung’ali Natural Resources Co. Ltd. Wakala wa Nishati Vijijini (REA) unafadhili Mradi huu ili kuwezesha kuongeza umeme katika gridi ya taifa. Taswira hii ilichukuliwa Septemba 23, 2023 wakati wa ziara ya Mkurugenzi wa Teknolojia za Nishati Jadidifu na Nishati Mbadala kutoka REA, Mhandisi Advera Mwijage.
Kutoka kushoto ni Mkurugenzi wa Teknolojia za Nishati Jadidifu na Nishati Mbadala kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Advera Mwijage, Mwenyekiti wa Kijiji cha Idete, Henry Lekuti na Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Lung’ali Natural Resources, Padre Luciano Mpoma wakijadili jambo wakati walipokuwa wakikagua maendeleo ya utekelezaji wa Mradi wa ujenzi wa umeme wa maji (kilovoti 2400) wa Idete wilayani Kilolo unaotekelezwa na Kampuni ya Lung’ali, Septemba 23, 2023. REA inafadhili Mradi huu ili kuwezesha kuongeza umeme katika gridi ya taifa.
Mkurugenzi wa Teknolojia za Nishati Jadidifu na Nishati Mbadala kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Advera Mwijage (katikati) akiwa na Mwenyekiti wa Kijiji cha Idete, Henry Lekuti (kushoto) na Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Lung’ali Natural Resources, Padre Luciano Mpoma wakikagua maendeleo ya utekelezaji wa Mradi wa ujenzi wa umeme wa maji (kilovoti 2400) wa Idete wilayani Kilolo unaotekelezwa na Kampuni ya Lung’ali, Septemba 23, 2023. REA inafadhili Mradi huu ili kuwezesha kuongeza umeme katika gridi ya taifa.

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages