Breaking

Sunday 31 March 2024

AIR TANZANIA YASHEREHEKEA PASAKA KWA KUZINDUA SAFARI YA DUBAI

Dar es Salaam, 31 Machi 2024

Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL) imezindua safari za moja kwa moja kwenda nchi za Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE). Hafla hiyo imefanyika katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar es Salaam Terminal 3.

Kampuni ya Ndege inaongeza wigo wa mtandao wake wa safari za kimataifa kwa kuanzisha safari za kutoka Dar es Salaam hadi Dubai, kuanzia Machi 31, 2024.

Safari za ndege za moja kwa moja kwenda Dubai zitafanyika mara nne kwa wiki kwa kutumia ndege yake mpya ya kisasa kabisa B737-9 MAX ambayo ina viti 181 vya abiria ambapo viti 16 Daraja la Biashara na viti 165 Daraja la Kawaida. Safari hii itachukua takriban saa 5 na dakika 30.

Kuanzishwa kwa safari za Dubai ni miongoni mwa utekelezaji wa Mkakati wa Biashara wa ATCL wa kuunganisha mtandao wake wa safari kwenye masoko makubwa duniani.

"Kama sehemu ya mkakati wetu wa kuongeza wigo wa safari, tunafurahi kuungana na mashirika makubwa ya ndege duniani katika kuwezesha safari za Dubai kwa sababu ni mkakati wa muda mrefu ambao unapanua wigo wa safari na kutoa fursa zaidi za uchaguzi kwa abiria wetu. Abiria wetu watapata uzoefu wa pekee wakati wa safari pamoja na kuona thamani ya fedha zao”, amesema Mkurugenzi Mtendaji, Eng. Ladislaus Matindi.

Uzinduzi wa safari ya Dubai ni kudhihirisha dhamira yetu na uwezo wetu kuhudumia masoko ya kimataifa ambayo yanatoa fursa nyingi za biashara na utalii kwa wateja”, aliongeza Mhandisi Matindi.

Tiketi zimeanza kuuzwa kwa nauli ya punguzo maalum ambayo inaanzia $399 kwenda na kurudi ambapo abiria atapewa idhini ya kusafiri na mabegi matatu (3) kila begi kilo 23 kwa daraja la kawaida na kilo 30 kwa daraja la biashara.

Air Tanzania inawaalika mawakala wa usafiri na wale wa watalii kuchangamkia fursa mbalimbali zilizopo kwa kufanya biashara pamoja.

Kampuni ya Ndege Tanzania ina miliki ndege aina ya B787- 8 Dreamliners, A220-300, B737- 9 MAX, Q400 na B767-300F.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: +255 621 896 990

Pages