Breaking

Monday 11 March 2024

DAWASA YABORESHA MIUNDOMBINU USAMBAZAJI MAJI KIBAMBA, KISARAWE

Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es salaam (DAWASA) inaendelea na zoezi la maboresho ya kituo cha kusukuma maji Kibamba ambapo zoezi hilo limehusisha ufungaji wa pampu mpya yenye uwezo wa kusukuma maji lita laki 2 kwa saa na ufungaji wa transfoma kubwa yenye uwezo wa kutoa umeme wa kilovoti 1000 kutoka kilovoti 500 iliyokuwepo awali kwa lengo la kuongeza msuko wa maji na ufanisi wa kituo hicho.

Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA Ndugu Kiula Kingu wakati akikagua kazi hiyo amesema maboresho haya yataenda kuondoa changamoto ya upatikanaji wa maji kwani kwa kuongeza msukumo wa maji na hivyo kutawezesha kujaza tenki la Kisarawe lililokuwa linachukua muda wa saa 32 kujaa lakini baada ya maboresho tenki hilo litajaa kwa muda wa chini ya saa 12 na hivyo kuimarisha huduma ya upatikanaji wa maji kwa wakazi wa majimbo manne ya uchaguzi jimbo la Ukonga, Kisarawe, Segerea na sehemu ya jimbo la Ilala

"Maboresho haya yataenda kuleta mabadiliko chanya katika huduma hivyo niwatoe hofu wakazi wote wa maeneo haya kwamba maji yatapatikana na kwa uhakika zaidi, Kazi inaendelea na tunategemea kuimaliza kwa wakati" amesema Ndugu Kiula

Naye Mwenyekiti wa Serikali ya mtaa Kazumzimbwi Ndugu Amini Kidete ameishukuru Serikali kupitia DAWASA kwa kufanya maboresho kwenye kituo hicho ambayo yataenda kuondoka changamoto ya msukumo mdogo kwa maeneo mengi katika mji wa Kisarawe mtaa wake ukiwa mmoja wapo.

"Tunaishukuru Serikali yetu kilio kikubwa kwa wananchi ni huduma bora ya maji ikiwa imepewa kipaumbele kikubwa kama hivi sisi tunapata ahueni tunawaomba wamalize kwa haraka ili huduma ianze kupatikana" amesema Ndugu Kidete.







Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages