Breaking

Thursday 25 April 2024

KISOPWA KUNUFAIKA MRADI WA KISASA WA KUCHAKATA MAJITAKA

Wakazi wa mtaa wa Kisopwa katika kata ya Kiluvya Wilayani Kisarawe wanatarajia kuwa wanufaika wa kwanza wa utekelezaji mradi wa ujenzi wa mitambo ya kuchakata majitaka inayojengea na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es salaam (DAWASA) utakaoboresha afya za wakazi takribani 3,500

Akizungumza na viongozi na watendaji wa Serikali za Mitaa na Kata, Afisa maendeleo ya jamii DAWASA ndugu, Vivian Silayo wakati wa kutambulisha mwongozo wa kushughulikia malalamiko wakati wa utekelezaji wa miradi hiyo na kuwataka viongozi hao kuonyesha ushirikiano ili mradi ulete manufaa yaliyotarajiwa.

"Mtambo huu wa kuchakata majitaka ni wa kisasa na bora sana katika jamii hi ya wana kisopwa, tunategemea kukamilika kwake kutaboresha usafi wa mazingira zaidi katika mtaa wa Kisopwa na Kata ya Kiluvya na tunatambulisha muongozo wa kushughulikia malalamiko wakati wa utekelezaji wa mradi ili kuhakikisha unakamilika kwa wakati bila changamoto." ameeleza Silayo

Silayo ameongeza kuwa muongozo huu unamanufaa mengi wakati wa utekelezaji wa mradi kama vile upatikanaji wa haraka kwa malalamiko kwa njia rahisi na shirikishi, kutambua na kupata ufumbuzi wa masuala yanayoweza kuathiri mradi na jamii kwa ujumla.

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Kiluvya Mheshimiwa Aidan Kitare ameishukuru DAWASA kwa kuendelea kuleta miradi katika kata hiyo na kuahidi ushirikiano mkubwa kuhakikisha mradi huu unakamilika kwa wakati.

"Wilaya ya Kisarawe ina kata 17, lakini Kiluvya ina bahati kubwa kupata mradi huu tena katika mtaa wa Kisopwa, niwaombe Wananchi kutoa ushirikiano wa kutosha na kutoleta sababu zozote zitazokwamisha ukamilishaji wa mradi huu kwa wakati." ameeleza Mhe. Kitare.

Muongozo wa kushughulikia malalamiko wakati wa utekelezaji wa mradi hutolewa ili kuhakikisha changamoto zinazojitokeza zinapatiwa ufumbuzi na muongozo huo hutumika pia kama njia shirikishi na ya pamoja katika kuleta suluhu na kufanikisha ukamilishaji wa mradi kutekelezwa ndani ya muda uliopangwa.



Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages