Breaking

Friday 3 June 2022

NESI MSAIDIZI AKUTWA NA KILO 174.77 ZA DAWA ZA KULEVYA AINA YA HEROINE - DAR





KAMISHNA Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya nchini (DCEA),Gerald Musabila Kusaya amesema, mamlaka hiyo imemkamata nesi msaidizi, Bw.Salum Shaban mkazi wa Tabata Relini katika Halmashauri ya Manispaa ya Ilala, Dar es Salaam akiwa na kilo 174.77 za Dawa za Kulevya aina ya Heroine.


Ameyasema hayo leo Juni 3,2022 wakati akitoa taarifa kuhusu mambo mbalimbali yaliyofanywa na mamlaka hiyo kwa kipindi cha Januari hadi Mei, 2022.


"Bwana Salum Shaban ambaye ni nesi msaidizi katika zahanati moja huko Kariakoo alikamatwa Mei 12, 2022 nyumbani kwake huko Tabata Relini akiwa ameweka kilo 174.77 za dawa za kulevya zikiwa juu ya kitanda chake, huku yeye akiwa amelala chini,"amesema Kusaya.


Ameongeza kuwa Kufuatia upekuzi uliofanyika nyumbani kwa mtuhumiwa, paketi 162 zenye unga uliodhaniwa dawa za kulevya zilikutwa ndani ya viroba sita vilivyokuwa vimehifadhiwa chumbani kwa mtuhumiwa.


Amesema kuwa taarifa ya uchunguzi wa kitaalam kutoka kwa Mkemia Mkuu wa Serikali imethibitisha kuwa paketi zote 163 zilikuwa na dawa za kulevya aina ya heroin ambazo jumla yake ni Kilogramu 174.77.


Mtuhumiwa atafikishwa mahakamani mara baada ya taratibu za kisheria kukamilika.


Katika hatua nyingine Kusaya amesema
Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya imekamata jumla ya kilogramu 877.217 za dawa za kulevya na kuzuia uingizaji wa kilogramu 122,047.085 na Lita 85 za kemikali bashirifu Nchini.


Amebainisha kuwa Dawa za hizo ni heroin kilogramu 174.112 zilizowahusisha watuhumiwa wawili na bangi kilogramu 703.105 zilizowahusisha watuhumiwa sita ambao wote wamefikishwa mahakamani.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages