Breaking

Monday 12 September 2022

UWANJA WA BASHUNGWA WAANZA KUJENGWA, TAA ZA BARABARANI ZINAENDELEA KUFUNGWA KARAGWE



OR-TAMISEMI

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI) Mhe. Innocent Bashungwa amewahakikishia wananchi wa Wilaya Karagwe kuwa atahakikisha anatimiza ahadi yake ya kujenga kwa kuweka uzio wa uwanja wa mpira wa Wilaya maarufu kwa jina la Bashungwa Stadium.

Ameyasema hayo Septemba 11, 2022 katika fanali za ligi ya mpira wa miguu ya Bashungwa Karagwe Cup 2022 iliyofanyika katika uwanja huo ambao umeshaanza kujengewa msingi ili kuwekewa uzio wa ukuta na kufanyiwa maboresho.

“Niwaahidi Wanakaragwe, itakapofika mwaka kesho katika fainali za ligi ya Bashungwa Cup, uwanja huu utakuwa umeshajengwa kwa kuzungusha ukuta na kufanyiwa Maboresho na kuwa na hadhi ya uwanja wa Wilaya,” amesema Mhe.Bashungwa ambaye pia ni Mbunge wa Karagwe.

Bashungwa ameeleza kuwa uwanja huo wa Wilaya ukijengewa uzio utatoa fursa kwa wananchi kwa kuletwa matamasha mbalimbali na wasanii wakubwa kufanya maonesho ya mziki ambayo yalikuwa hayafanyiki wilayani humo.

Aidha, Waziri Bashungwa amemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kumuwezesha kutimiza ahadi yake ya kufunga taa za barabarani katika Mamlaka ya Mji mdogo wa Kayanga na Omurushaka ambapo kazi hiyo ya ufungaji wa taa inaendelea.

Amesema ufungaji wa taa za barabarani utaendelea katika mitaa, ambapo TARURA wanaendelea na taratibu za kupata Mkandarasi wa kutekeleza kazi hiyo katika mitaa ya Mji wa Kayanga na Omurushaka wilayani Karagwe.

Vile vile, Bashungwa amesema mchakato wa ujenzi wa stendi ya kisasa ya Wilaya unaendelea ambapo Rais Samia ameshatoa fedha ili kukamilisha mradi huo uliosubiriwa kwa muda mrefu.

Kwa Upande Wake, Waziri wa Maji Mhe. Jumaa Aweso amempongeza Waziri Bashungwa kwa kuendelea kuwatumikia kikamilifu wananchi wa jimbo hilo na kumsaidia Rais Samia katika Wizara ya TAMISEMI.

Ligi ya Mpira ya Bashungwa Karagwe Cup inafanyika kila mwaka kwa kuzikutanisha timu za mpira za kata zote 23 za Wilaya Karagwe ambapo mwaka huu timu ya Kata Nyabiyonza imetwaa ubigwa, ikifuatiwa na Kayanga mshindiwa pili, Kiruruma Mshindi wa tatu na Chanika Mshindi wa nne.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages