Breaking

Sunday 23 October 2022

WANANCHI WAPEWE ELIMU JUU YA MRADI WA UMWAGILIAJI



Na Lucas Raphael,Tabora

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Mbegu za Kilimo ASA Dkt. Sophia Kashenge ameuomba uongozi wa Mkoa wa Tabora na Wilaya ya Nzega kusaidia kutoa Elimu kwa Wananchi waishio pembezoni mwa Shamba la Mbegu Kilimi Nzega linalotarajiwa kuwekewa miundombinu ya Umwagiliaji hivi Karibuni.

Akizungumza na Katibu Tawala wa Mkoa wa Tabora Dkt..John Mboya, Mtendaji Mkuu wa Wakala Dkt.. Sophia Kashenge Alisema wananchi wanapaswa kupewa Elimu juu ya umuhimu wa Umwagiliaji katika sekta ya kilimo iliwaweze kuwa walinzi wa miundombinu itakayowekwa

Alisema Serikali imewekeza fedha nyingi katika sekta ya Kilimo hasa katika Umwagiliaji hivyo viongozi wanapaswa kusaidiana kuelimisha wananchi waweze kuelewa.

"Miundo mbinu hii ya umwagiliaji wa aina hiyo ya mabomba ya mvua (centre pivot) haifahamki kwa wengi na Kwa kuwa ni teknolojia ngeni Kwa wengi wetu na jinsi ulivyo ni rahisi sana Kwa baadhi ya watu na watoto watundu kuichezea na kutaka kujaribu mambo mbalimbali ikiwemo kupanda katika mabomba na hata kuichezea na wakati mwingine wengine kujaribu kupata baadhi ya vyuma Kwa matumizi mengine. “alisema Dkt..Sophia

Alisema kwamba “Kwa kweli itasikitisha kuona baadhi ya jamii inaharibu miundombinu hii ambayo Serikali imetumia fedha nyingi kuwekeza kwa lengo la Kuongeza Uzalishaji wa Mbegu Nchini. Ni matumaini yetu tutashirikiana kutoa Elimu kwa jamii yetu Ili mradi huu uweze kuleta mabadiliko katika sekta ya kilimo".Dkt.sophia Alisema hayo mbele ya Katibu tawala Mkoa wa Tabora.

Dkt.Sophia alisema Serikali kupitia Wakala wa Mbegu za Kilimo ASA imetenga Billion 18 kuweka miundombinu ya aina hiyo ya Umwagiliaji katika mashamba matatu ya Wakala.

Akitaja mashamba hayo alisema Shamba la Msimba Kilosa Mkoani Morogoro litawekewa miundombinu hekta 200 sawa na Ekari 500,Shamba la Ngaramtoni Arusha hekta 200 sawa na Ekari 500 huku Shamba la Kilimi hekta 400 sawa na Ekari 1000.

Aidha alisema Miradi hiyo yote mitatu itajengwa na wakandarasi vijana wazawa ambao ni Kampuni ya Pro Agro Grobla Ltd ya Jijini Arusha.



Kwa upande wake Katibu Tawala Mkoa wa Dkt.John Mboya alisema kama Mkoa wa Tabora utahakikisha unatoa Elimu kwa jamii ya Nzega hata waishio pembezoni mwa Shamba iliwaweze kulinda miundombinu hiyo.
Alisema Serikali ya Mkoa inawapongeza ASA kupitia Wizara ya Kilimo kwa kuanza kuweka miundombinu ya Umwagiliaji kwa mashamba matatu ya Wakala ilikuongeza tija ya kilimo pamoja na Uzalishaji wa Mbegu bora.

Aliwataka wananchi wa Nzega kutoa ushirikiano kwa Serikali katika Miradi hiyo Mikubwa inayoanza na Ile inayoendelea kutekelezwa.

Alisema kukamilika kwa mradi huo wa Umwagiliaji wenye hekta 400 sawa na Ekari 1000 utaongeza upatikanaji wa ajira kwa jamii inayozunguka Shamba wakiwemo kina mama, vijana na hasa mafundi mitambo pamoja na kazi mbalimbali katika mnyororo wa uzalishaji wa mbegu za Kilimo.

Mwisho.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages