Breaking

Friday 28 October 2022

WANANCHI WATAKIWA KUACHA KUKATA MITI, KUVAMIA MAENEO YA HIFADHI



Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe.Mary Masanja (MB) amewataka wakazi mkoani Njombe kuwa Wahifadhi kwa kuacha tabia ya kukata miti ovyo na kuepuka kuvamia maeneo ya hifadhi.

Ameyasema hayo Oktoba 27,2022 katika ziara ya Mawaziri wa Kisekta ya kutatua migogoro ya ardhi kwenye Kijiji cha Mpanga, Wilaya ya Wanging'ombe Mkoani Njombe.

“Niwaombe tulilinde Pori la Akiba la Mpanga Kipengere, tuwe wahifadhi wazuri, tusiende kukata miti hovyo, tusiingie ndani na kuvamia vyanzo vya maji kwa sababu vinasaidia upatikanaji wa maji safi na salama” amesema.

Naibu Waziri Masanja amewatahadharisha wananchi kutoyasogelea maeneo ya Hifadhi kwa kuwa yana wanyamapori ambao ni hatari kwa binadamu.

Pia, amewaasa kuacha mtindo mbaya wa kusafisha mashamba kwa kuchoma moto,ili kuepuka moto kusambaa katika mashamba ya miti.

Ziara ya Kamati ya Mawaziri wa Kisekta imemalizika mkoani Njombe ambapo itaendelea na shughuli za utatuzi wa migogoro ya ardhi Oktoba 28,2022 Mkoani Ruvuma.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages