Breaking

Wednesday 30 November 2022

WATATU WAKAMATWA TUHUMA ZA KUMZIKA MTOTO WA MIEZI MIWILI AKIWA HAI" WALIMTOA KAFARA ILI WATAJIRIKE"




Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza limefanikiwa kuwakamata watuhumiwa watatu wa makosa ya mauaji ya mtoto wa miezi miwili yaliyotokana na imani za kishirikina.

Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza SACP Wilbroad Mutafungwa ameeleza kuwa tukio hilo la kikatili limetokea Novemba 13, 2022 mchana katika mtaa wa Kisundi, kata ya Bugogwa, Wilaya ya ilemela ambapo Zawadi Msagaja (20) aliyekuwa akiishi kwa dada yake aliamriwa na shemeji yake aitwaye Mussa Mazuri ambaye ni mganga wa kienyeji kumtoa kafara mtoto wake wa kike Neema Claud mwenye umri wa miezi miwili ili wapate utajiri na endapo akikataa atamtoa yeye kafara.

Kamanda Mutafungwa amesema kuwa mwanamke huyo inadaiwa alikubali kumtoa mtoto wake kafara ili yeye asife ndipo mganga huyo kwa kushirikiana na mkewe aitwaye Elizabeth Kaswa walianza kumpa dawa za kienyeji mtoto ambapo alianza kuishiwa nguvu.

Ilipofika Muda wa saa 20:00 usiku wote watatu wakiwa na mtoto huya walikwenda shambani na kuchimba shimo kisha kumzika akiwa hai na baadae walirudi nyumbani

"Jeshi la Polisi lilipata taarifa toka kwa wasamaria wema kuhusiana na tukio hilo ndipo ufuatiliaji wa haraka ulifanyika na kufanikiwa kumkamata mama wa mtoto huyo aitwaye Zawadi Michael Msagaja pamoja na dada yake Elizabeth John Kaswa, na tarehe 21.11.2022 mtuhumiwa Musa James Mazuri, miaka 31, mkazi wasamba B, alikamatwa huko kijiji cha Nyanguge Wilayani Magu" ameeleza SACP Mutafungwa

askari waliongozana na mama wa mtoto hadi eneo la tukio na kufukua kaburi na kufanikiwa kuukuta mwili wa mtoto aliyezikwa akiwa hai ukiwa umefungwa kanga ambapo mwili wa mtoto uljpelekwa hospitali ya Rufaa ya Bugando kusubiri uchunguzi wa daktari.

"Upelelezi wa shauri hili unakamiljshwa haraka iwezekanavyo na watuhumiwa wote watafikishwa mahakamani kukabiliana na mkono wa sheria" amesema kamanda Mutafungwa

Aidha Kamanda Mutafungwa ametoa Wito kwa wananchi kuacha imani potofu za kishirikina ambazo zimekua zikipoteza maisha ya watu na wengine kuingia kwenye matatizo ya vifungo vya maisha jela.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages