Breaking

Thursday 15 December 2022

WANANCHI WALIOVAMIA MSITU WILAYANI MVOMERO WATAKIWA KUONDOKA




Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) amewataka wananchi waliovamia hifadhi ya Msitu wa Kuni na kuanzisha shughuli za ujenzi wa nyumba katika hifadhi hiyo wasitishe na kuondoka mara moja katika eneo hilo ili kulinda ikolojia ya eneo.

Ameyasema hayo leo alipokuwa akizungumza na wananchi katika Wilaya ya Mvomero Mkoani Morogoro.

“Sasa tunachowaomba kwanza msimamishe ujenzi kwenye eneo la msitu ,pili tutaangalia wale ambao wamejimilikisha maeneo makubwa ili tuyagawe kwa sababu wote ni wavamizi” amesisitiza Mhe. Masanja.

Amesema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa huruma yake aliruhusu eneo la msitu lenye jumla ya hekta 2000 limegwe ili kugawiwa kwa wananchi lakini wananchi mmeendelea kulivamia eneo la msitu.

“Mwaka jana tulielekeza wananchi wapangwe kwenye hekta elfu 2000 na hiyo ni huruma ya Mheshimiwa Rais Samia, naomba tumpongeze Mama yetu ana huruma kwa sababu ilikuwa muondolewe lakini akasema hapana hawa ni wananchi wangu wapangwe” Amesisitiza Mhe. Masanja.

Ameeleza kuwa wananchi waliomo kwenye hekta elfu 2000 zilizomegwa wakagawiwa wako kihalali na watapimiwa ardhi na kupewa hati zao lakini waliovamia wanapaswa kuondoka katika eneo hilo.

Msitu wa Kuni unaomilikiwa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) ulisajiliwa mwaka 1953 kwa tangazo la Gazeti la Serikali.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages