Breaking

Saturday 21 January 2023

TFS MANYONI WATAKIWA KUHAMASISHA WANANCHI KUJIUNGA NA MIRADI YA UFUGAJI NYUKI



Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Wilaya ya Manyoni imetakiwa kuelimisha jamii juu ya umuhimu wa kujiunga na miradi ya ufugaji nyuki ili kuendeleza uhifadhi wa mazingira na kujiongezea kipato kutokana na mazao yatokanayo na ufugaji nyuki kama asali.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) wakati wa kikao na watumishi wa TFS kilichofanyika januari 20,2023 wilayani Manyoni mkoani Singida.

‘Wajibu wenu ni kutoa elimu kuhusu umuhimu wa uhifadhi ili jamii ielewe na muwe na programu zinazooneshwa kwenye luninga kuelimisha jamii. Pia muhakikishe asilimia kubwa ya wawekezaji kwenye miradi ya ufugaji nyuki wawe ni wananchi wa kawaida ili kuwafanya wasikate miti” amesisitiza Mhe. Masanja.


Aidha, amewataka wahifadhi kuendelea kutoa elimu kuhusu umuhimu wa Uhifadhi kuanzia ngazi ya uongozi wa Wilaya na Mkoa hasa wakati wa ufunguzi wa mashamba ili kuwepo na uhifadhi endelevu.

Naye, Mhifadhi Mkuu Shamba la Nyuki Manyoni, Hashimu Gau amesema madhumuni ya kuanzisha hifadhi hiyo ni kulinda ikolojia ya Itigi ambayo ni maarufu kwa kuzalisha mazalia ya nyuki, eneo hilo pia hutumiwa na jamii kwa kutundika mizinga yao hivyo kujipatia kipato na ajira za muda mfupi za usafishaji mipaka ulinzi na usafi wa mizinga.

Amesema Hifadhi ya Nyuki ya Taifa ya Aghondi ina jumla la Manzuki 7 ambazo kati ya hizo 5 ni za TFS na mbili za wadau zikiwa na jumla ya mizinga 581 ambapo kati ya hiyo mizinga 331 ni ya TFS na 252 ya wadau.

Ziara hiyo ni utekelezaji wa majukumu yake ya kusimamia maeneo ya hifadhi na kuhamasisha miradi ya ufugaji nyuki.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages