Breaking

Tuesday 31 January 2023

WANNE WATUPWA JELA MIAKA 120



Na Abel Paul wa Jeshi la Polisi

JESHI la Polisi Mkoa wa Arusha limesema katika kukahakikisha linakomesha vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia na Watoto limeendelea kushirikisha jamii na kutoa elimu ambapo limebainisha kuwa mkakati waliojiwekea umesaidia Jeshi hilo na ofisi ya Taifa ya Mashtaka mkoani humo kuwafikisha mahakamani watuhumiwa wanne na mahakama kuwakuta na hatia kwa makosa ya ubakaji.

Akitoa taarifa hiyo mapema leo Januari 31,2023 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha Kamishina msaidizi wa Polisi ACP JUSTINE MASEJO amewataja waliofikishwa mahakamani kuwa ni JAMES ELIREHEMA, JOHN SANARE, THEOPHILI SALAHO, JAPHET MUNGURE ambapo mahakama hiyo iliwakuta na hatia na iliwahukumu kifungo cha miaka (30) kwenda Jela kila mmoja kwa kosa la ubakaji.

Kamanda Masejo aliendelea kusema kuwa katika kuhakikisha Jeshi hilo linaendelea kufuatilia vitendo vya ukatili wa Watoto unaofanywa na baadhi ya watu katika Mkoa huo amesema Jeshi hilo lilifanikiwa kumkamata DOREEN LEMA (30) mkazi wa Baraa katika halmashauri ya jiji la Arusha kwa kosa la kumchoma pasi ya umeme mtoto wake wa kumzaa mwenye umri wa miaka saba katika maeneo mbalimbali ya mwili wake.

Ameeleza kuwa mtuhumiwa huyo alikamatwa na alifikishwa katika mahakama ya hakimu mkazi wilaya ya Arusha ambapo alikutwa na hatia na kuhukumiwa kifungo cha miaka mitano (05) Kwenda jela kwa kosa la kumchoma mtoto na pasi.

Pia katika tukio jingine kamanda Masejo amesema kuwa Jeshi hilo limefanikiwa kukamata pikipiki iliyokuwa imeibiwa huko katika Kijiji cha Qangadend wilaya ya Karatu ambapo mtuhumiwa CHARLES JONAS (27) mkazi wa Igunga Mkoani Tabora alikamatwa akiwa na pikipiki yenye namba za usajili SM 12337 aina ya Boxer Mali ya serikali ya Jamhuri ya Tanzania.

Aidha uchunguzi wa tukio hilo ulifanyika na mtuhumiwa alifikishwa katika mahakama ya wilaya Karatu na kusomewa mashtaka yanayomkabili ambapo mahakama ilimkuta na hatia na kumhukumu kifungo cha miaka mitatu jela.

ACP Masejo ametoa wito kwa wananchi kutojihusisha na vitendo vya ukatili wa aina yoyote ile kwani Jeshi la Polisi Mkoani hapa halito muonea muhali mtu yoyote atakaye bainika kwa makosa ya unyanyasaji vilele Jeshi la Polisi linawaomba wananchi kuendelea kutoa taarifa za vitendo hivyo Pamoja na uhalifu na wahalifu katika Mkoa wetu.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages