Breaking

Friday 17 February 2023

WAZIRI DKT MABULA ATAKA MOTISHA OFISI ZINAZOFANYA VIZURI MAKUSANYO YA ARDHI



Na Munir Shemweta, WANMM MOROGORO

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi ametaka kuandaliwa utaratibu utakaotoa motisha kwa ofisi za ardhi zitakazofanya vizuri katika ukusanyaji mapato yatokanayo na kodi ya pango la ardhi ili kuleta ushindani.


Aidha, ametaka ofisi za ardhi katika mikoa na halmashauri nchini kuhakikisha zinatumia fursa ya Msamaha wa Riba ya Malimbikizo ya Kodi ya Pango la Ardhi uliotolewa na mhe Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kuhamasisha wananchi wanaodaiwa kulipa kodi hiyo katika muda uliotolewa.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ametoa msamaha wa riba ya malimbikizo ya kodi ya pango la ardhi kwa wadaiwa kulipa deni la msingi kufikia April 30, 2023.


Dkt Mabula amesema hayo tarehe 16 Februari 2023 mkoani Morogoro katika kikao kazi cha Menejimenti ya Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi na Makamishna wa Ardhi Wasaidizi wa Mikoa katika maandalizi ya Bajeti ya Wizara kwa mwaka 2023/2024.


‘’Ni vizuri katika kuhamasisha ukusanyaji mapato yatokanayo na kodi ya pango la ardhi tukaangalia namna bora ya kutoa motisha kwa zile ofisi za ardhi zinazofanya vizuri, hii itasaidia kuongeza mapato’’ alisema Dkt Mabula.


Akigeukia Msamaha wa Riba ya Malimbikizo ya Kodi ya Pango la Ardhi uliotolewa na mhe. Rais Dkt Mabula alisema anataka kuona kila mkoa 'unachacharika’ kuhakikisha kunakuwa na ushindani wa kuhamasisha watu kulipa kodi.


‘’Nataka kuona kila mkoa unachaharika maana ni aibu msamaha unatolewa halafu tunakusanya kidogo, tutumie fursa ya msamaha wa Rais kuhamasisha wananchi na taasisi kulipa kodi ya pango la ardhi’’ alisema Dkt Mabula.


Aidha, Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi alitumia fursa ya kikao kazi cha Wizara kutaka kuona malengo ya ukusanyaji mapato ya kodi ya ardhi yanakuwa na uhalisia badala ya kujiwekea malengo makubwa anayokinzana na hali halisi.


‘’Malengo yetu ya ukusanyaji mapato ya ardhi walau yasiwe yanakinzana na uhalisia kwa kujipa matumaini ya kukusanya kiasi kikubwa wakati uhalisia ni kukusanya kidogo’’ alisema Dkt Mabula.


Waziri Dkt Mabula pia alielezea suala la Klinik za Ardhi ambapo ametaka kupatiwa taarifa ya mikoa iliyotokeleza kazi hiyo kwa muda gani kutokana na kazi hiyo kuonesha kulegalega huku akibainisha kuwa, Kliniki hizo za Ardhi zinasaidia sana kutatua migogoro ya ardhi.


Klinik za Ardhi ni utaratibu ulioanzishwa na Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi ambapo kila mkoa unakuwa na Kituo Jumuishi kwa siku maalum na kutoa huduma mbalimbali za sekta ya ardhi pamoja na kusikiliza kero za wananchi .


Pia Waziri Dkt Mabula aliagiza Wakurugenzi wa Wizara yake kutoka kwenda kwenye mikoa kuona kazi za idara husika zinavvyofanyika kwa lengo la kufahamu changamoto zilizopo na kusisitiza kuwa, utaratibu huo kutumika katika ngazi za mikoa kushuka chini na kubainisha kuwa bila kufanya hivyo kazi hazitafanyika kwa ukamilifu.


Katka kuhitimisha maagizo yake katika kikao hicho, Dkt Mabula ametaka ushirikiano wa ofisi za ardhi za mikoa na zile za halamashauri kwa kutekeleza yale waliyokubaliana na kuwataka watendaji kutosubiri kuitwa katika matatizo na kusisitiza kutumia vikao kutoa ushauri kwa halmashauri.


Kikao Kazi cha Menejimenti ya Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi na Makamishna wa Ardhi Wasaidizi wa Mikoa kinafanyika kwa siku tatu kuanzia tarehe 15-17 Februari 2023 mkoani Morogoro ambapo pamoja na mambo mengine kinajadili Bajati ya Wizara hiyo kwa mwaka ujao wa fedha 2023/2023.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages