Breaking

Thursday 2 March 2023

NDEJEMBI ATOA MIEZI MIWILI SHULE YA WASICHANA SINGIDA KUKAMILIKA , AAGIZA TAKUKURU KUFANYA UCHUNGUZI



OR -TAMISEMI

Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Deogratius Ndejembi (Mb) ametoa miezi miwili  kwa Mkurungenzi wa Halmashauri ya Manyoni kukamilisha ujenzi miundombinu yote ya shule maalum ya Sayansi ya Wasichana ya Mkoa wa Singida.

Ametoa maelekezo hayo tarehe 01 Machi, 2023 wakati alipofanya ziara ya kukagua shule ya sayansi ya kidato cha kwanza hadi cha sita inayojengwa Solya Wilaya ya Manyoni kwa gharama ya  shilingi bilioni tatu (3,000,000,000).


Mhe. Ndejembi amebaini mapungufu katika usimamizi wa ujenzi wa shule hiyo ikiwa ni pamoja na kutofuatwa mwongozo wa manunuzi na taratibu za malipo kwa Makandarasi wanaoendelea na ujenzi.


Amemuagiza Afisa wa TAKUKURU wilaya ya Manyoni  ndani ya siku saba kufanya uchunguzi na kuwasilisha Ofisi ya Rais - TAMISEMI juu mapungufu aliyoyabaini katika ujenzi wa shule hiyo ili hatua sitahiki zichukuliwe.


Aidha, Mhe. Ndejembi amemuagiza Mkurungenzi wa Halmashauri kuwachukulia hatua za kinidhamu afisa manunuzi na mhandisi kwa kufanya malipo kwa mkandarasi kinyume na taratibu ambapo malipo yalifanyika kabla ya kibali cha malipo kutolewa pomoja kununua vifaa zaidi ya BQ iliyoelekeza.


Mhe. Ndejembi amesema Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hasaan mwezi Januari, 2022 alitoa bilioni 3 za awamu ya kwanza  kujenga shule hiyo ambayo ilitakiwa kukamilika mwezi Desemba, 2022 na kuanza kupokea wanafunzi mwezi Januari mwaka huu lakini mpaka sasa ujenzi haujakamilika.


Mkoa wa Singida ni moja kati ya mikoa kumi nchini iliyopokea  kiasi cha shilingi bilioni tatu kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya za wasichana za mikoa ili kujenga vyumba vya madarasa 12, jengo la utawala 1, maabara 4, maktaba 1, matundu ya vyoo 16, chumba cha jenereta, bwalo, mabweni 5, mitaro ya maji, kichomea taka, matanki ya chini ya maji, matanki ya plastiki, uzio, njia za kutembelea na nyumba mbili za walimu.

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages