Breaking

Wednesday 31 May 2023

SERIKALI KUTATHMINI ENEO LA HIFADHI YA MSITU WA USUMBWA WILAYANI USHETU




Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii imesema itafanya tathmini ya Hifadhi ya Msitu wa Usumbwa iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu Mkoani Shinyanga, kwa lengo la kujiridhisha kama eneo hilo linastahili kumegwa kwa ajili ya kutengwa eneo la kuchungia mifugo ya wananchi.


Hayo yamesemwa leo Mei 31,2023 na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Ushetu, Mhe. Peter Cherehani aliyetaka kujua lini Serikali itatenga maeneo ya kuchungia mifugo katika pori la Usumbwa Forest Reserve.


Amesema Serikali inatambua mahitaji ya wananchi wa Ushetu hivyo pindi tathmini itakapokamilika wananchi watajulishwa.


Aidha amewataka wananchi wa Ushetu kuendelea  kuheshimu maeneo ya msitu kwa maslahi mapana ya Taifa.


Kuhusu Mgogoro wa mipaka kati ya Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania na Halmashauri, Mhe. Masanja amesema hakuna haja ya kugombania mipaka  isipokuwa ni masuala ya kiutawala ya kuelewana.


"Kwa kuwa sisi sote ni Serikali hakuna haja ya kugombana   tukae pamoja tuangalie namna ya kuainisha mipaka ili sisi sote tulinde haya mapori kwa pamoja" Mhe.Masanja amesisitiza.

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages