Breaking

Friday 29 December 2023

KC ZA HALMASHAURI YA WILAYA YA KINONDONI WACHAMBUA BAJETI YENYE MLENGO WA JINSIA

NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

MTANDAO wa Jinsia Tanzania (TGNP) kupitia Vituo Vya Taarifa na Maarifa Wilaya ya Kinondoni wamekutana na kuchambua bajeti yenye mlengo wa Jinsia ambapo bajeti hiyo wameangalia upande wa Afya, Miundombinu, Elimu na Maji.

Akizungumza leo Desemba 29,2023 Jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Kituo cha Taarifa na Maarifa Kata ya Mabwepande Bi.Fatma Nuri amesema kuwa Serikali imejitahidi kwenye upande wa afya kujenga vituo vya afya lakini baadhi ya vifaa bado havijakamilika.

Amesema kuwa upande wa elimu kuna baadhi ya changamoto kama vile upungufu wa vyoo kwa baadhi za shule zilizopo pembezoni mwa mji katika Wilaya hiyo.

“Vyoo vimejengwa lakini havijakamilika, kwa mfano shule ya Sekondari Mabwepande huu ni mwaka wa tatu vyoo bado havijakamilika na hatujui tatizo ni nini mpaka sasa”. Amesema Bi. Fatma.

Aidha amesema upande wa maji mashuleni bado ni changamoto hasa pembezoni mwa mji lakini kwenye upande wa miundombinu Serikali imejitahidi kutengeneza na kurekebisha baadhi ya barabara hasa katika maeneo ya pembezoni mwa mji.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Minazini Kata ya Makumbusho, Bw.Zuna Deogratius amesema wanategemea yale yote yaliyowasilishwa yatafanyiwa kazi kwa haraka ili wananchi waweze kupata huduma bora.

Naye Misago Goodluck kutoka Kituo Cha Taarifa na Maarifa Kata ya Makumbusho, amesema wameandaa yale waliyoyaona kwa mlengo wa kijinsia na kushirikiana na viongozi wa halmashauri ya Wilaya ya Kinondoni ili kuweza kulenga bajeti ya halmashauri hiyo yenye mlengo wa kijinsia.

Mratibu wa Masuala ya Maendeleo ya Kijinsia Manispaa ya Kinondoni Bi.Clara Urasa amesema kuwa wananchi wamekuwa na uelewa mkubwa kuhusu masuala ya kijinsia na maendeleo kwani wamepitia bajeti na kuona kuwa Manispaa ya Kinondoni imejitahidi kuangalia bajeti imelengaje Maendeleo ya kijinsia kwa pamoja.

“Pale ambapo wananchi wameona mapengo wametushauri tufanye nini, na sisi tumeyapokea na tunajaribu kupeleka kwa wahusika ili tuweze kufanya kazi ambayo wananchi wataipokea”. Amesema Bi. Clara.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages