Breaking

Friday 9 February 2024

WADAIWA SUGU HUDUMA ZA MAJI KORTINI

Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) imetoa muda wa siku 30 kwa wateja wenye malimbikizo ya muda mrefu wa bili za maji kulipa kabla hawajachukuliwa hatua za kisheria ikiwemo kuwafungulia mashtaka.

Afisa biashara Mkoa wa Kihuduma DAWASA Mlandizi Ndugu, Salome Stephano ameyasema hayo wakati akizungumza na wadaiwa hao na kusema kuwa Mamlaka inawataka wateja wenye malimbikizo ya muda mrefu mrefu wa zaidi ya siku 30 kujitahidi kulipa madeni yao mapema ndani ya muda kabla hatua za kisheria hazijachukuliwa.

Ameongeza kuwa pamekuwepo na wateja sugu wa muda mrefu wanaolimbikiza madeni yao kufikia miezi mitatu ambao na kutokana na hilo Mamlaka imewashtaki katika vyombo vya sheria.

"Mamlaka imefikia uamuzi wa kuwapeleka wadaiwa sugu Mahakamani kutokana na kulimbikiza madeni kwa muda mrefu licha ya kukumbushwa mara kwa mara kulipa, Mamlaka imewataka kulila bili zao na pia kwa wenye mkataba kuendelea kupunguza madeni yao kwa utaratibu uliowekwa na DAWASA ili kuondoa usumbufu wa mara kwa mara," ameeleza.

Lustic Paul mkazi wa Mtaa wa Mtongani amesema amekiri kuwa na deni la huduma za maji na kuahidi kulipa ndani ya muda uliopangwa.

Amewasihi wateja wengine wenye malimbikizo ya muda mrefu kulipa ili kuisaidia Mamlaka kuendelea kufikisha huduma ya maji kwa maeneo mengine yasiyokuwa na huduma.

Mkoa wa kihuduma DAWASA Mlandizi inahudumia jumla ya kata 11 ambazo ni Kwala, Mlandizi, Mtambani Visiga, Mbwawa, Kawawa, Janga, Kilangalanga, Ruvu, Vigwaza na Mtongani



Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: +255 621 896 990

Pages