Breaking

Friday 12 April 2024

PEMBAMNAZI WAPATIWA ELIMU HUDUMA ZA DAWASA

Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) kupitia mkoa wa kihuduma Kigamboni imeendesha zoezi la kufuatilia malipo ya huduma za maji kwa wateja wenye madeni ya muda mrefu kupitia Ofisi ya Serikali ya mtaa Puna katika kata ya Pemba-Mnazi Wilaya ya Kigamboni.

Zoezi hilo lilienda sambamba na utoaji wa elimu ya matumizi sahihi ya maji, utunzaji na ulinzi wa miundombinu ya maji, umuhimu wa kulipa bili za maji kwa wakati pamoja na sheria zinazosimamia sekta ya Maji.

Akiendesha zoezi hilo Meneja wa mkoa wa kihuduma Kigamboni, Ndugu Tumain Muhondwa amesema kuwa elimu iliyotolewa kwa watendaji wa Serikali ya Mtaa ni kiungo muhimu katika kuwafikia wateja wenye madeni ya muda mrefu.

"Kupitia ofisi za watendaji wa Serikali za mtaa zinatupa nguvu sisi kama Mamlaka kuwafikia wananchi wengi ambao sio tu wana madeni ya muda mrefu lakini pia wale wenye changamoto za kihuduma kusikilizwa na kupatiwa ufumbuzi," alisema ndugu Muhondwa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Serikali ya mtaa wa Puna, Ndugu Matokea Hassan ameipongeza DAWASA kwa kufanya zoezi hilo la kutatua changamoto za huduma ya maji wa mtaa wake na kutoa wito kwa Wananchi kuendelea kuipa ushirikiano Mamlaka.



Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages