Breaking

Tuesday 12 April 2022

TUME YA MADINI YAJA NA MKAKATI WA UKUSANYAJI WA MADENI SEKTA YA MADINI


Na Mwandishi Wetu-Dar es Salaam 


Mkurugenzi wa Huduma za Tume, William Mtinya amesema kuwa Tume ya Madini imeandaa mikakati mbalimbali ya ukusanyaji wa madeni mbalimbali ya Serikali yatokanayo na ukusanyaji wa tozo ikiwemo kwenye shughuli za utafutaji, uchimbaji, uchenjuaji na biashara ya madini ili kuendelea kuvuka lengo la ukusanyaji wa maduhuli linalowekwa na Serikali.


Mtinya amesema hayo kupitia mahojiano maalum kwenye kikao cha maafisa fedha kutoka Tume ya Madini Makao Makuu na Ofisi za Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa kinachoendelea jijini Dar es Salaam  chenye lengo la kukusanya na kuandaa taarifa ya fedha kwa mwaka wa fedha 2021/2022  pamoja na kujiwekea mipango madhubuti ya kutekeleza kwa mwaka wa fedha 2022/2023, kubadilishana uzoefu na kujifunza mifumo mbalimbali ya malipo Serikalini.


Ameeleza mikakati hiyo kuwa ni pamoja na kuhamasisha wadau wa madini kulipa madeni kwa njia ambayo ni ya kirafiki sambamba na kutoa elimu kwenye maeneo ya uchimbaji na biashara ya madini kuhusu umuhimu wa kulipa kodi na tozo mbalimbali Serikalini.


"Wahasibu na maafisa fedha wanatakiwa kwa kushirikiana na maafisa madini wakazi wa mikoa kujenga mazingira mazuri ya ulipaji wa madeni kwa wachimbaji na wafanyabiashara wa madini kwa kukaa nao, kujadiliana nao na kuweka mikakati ya kulipa kwa awamu bila kuathiri shughuli zao za uzalishaji wa madini," amesema Mtinya



Kwa upande wake  Meneja wa Fedha na Uhasibu wa Tume ya Madini Mwagule Dickson, akisisitiza juu ya ukusanyaji wa madeni, amewataka maafisa madini wakazi wa mikoa kuendelea kutoa elimu kwa wachimbaji na wafanyabiashara kuhusu Sheria ya Madini na kanuni zake, usalama kwenye shughuli za uchimbaji wa madini, ushirikishwaji wa watanzania kwenye Sekta ya Madini, (Local Content) na utoaji wa huduma kwa jamii zinazozunguka migodi ya madini (CSR) ambapo itawezesha kuwa na uchimbaji salama na endelevu hivyo kuwezesha sekta kuchangia kwa kiwango kikubwa katika uchumi wa nchi.


Wakati huohuo wakizungumza kwa nyakati tofauti maafisa fedha wamepongeza hatua ya Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Yahya Samamba kuanza zoezi la uhamasishaji la ulipaji wa madeni kwenye Sekta ya madini na kusisitiza kuwa watakuwa mabalozi wazuri kwenye maeneo yao ya kazi kwenye kampeni ya uhamasishaji na kukusanya madeni.

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages