Breaking

Saturday 9 July 2022

AJALI YAUA ASKARI WAWILI WA JWTZ, YAJERUHI WANNE




Askari wawili wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) wa kikosi cha 825 KJ kambi ya Mtabila iliyopo wilayani Kasulu mkoani Kigoma, wamefariki dunia na wengine wanne kujeruhiwa baada ya gari walilokuwa wamepakia kuacha njia na kupinduka.

Akizungumzia ajali hiyo leo Julai 9, 2022 mjini hapa, Kaimua Kamanda wa Polisi mkoa wa Kigoma, Menrad Sindano amesema tukio hilo limetokea Julai 8, Mwaka huu, majira ya saa sita mchana katika eneo la Kidahwe, wilaya ya Kigoma, mkoani Kigoma.

Amesema gari aina ya Toyota Land Cruiser mali ya Jeshi la Wananchi ambalo lilikuwa likiendeshwa na askari is Ramadhani George, gari hiyo iliacha njia na kupinduka na kusababisha vifo vya askari wawili ambao ni Advent Peter (31) na Nicholaus Lonjino (31).

“Majeruhi ni askari wa nne ambao wamejeruhiwa sehemu mbalimbali za miili yao ambao ni Andrea Augustino, Ramadhani George, Manyama Fredrick na Ngongolima Misungwi ambapo kwasasa wote wanapatiwa matibabu katika hospitali ya rufaa ya mkoa Maweni,” amesema.

Amesema majira ya mchana siku ya leo majeruhi wote wanatarajiwa kusafirishwa kwa njia ya ndege kwenda hospitali ya kijeshi Lugalo jijini Dar es Salaam kwa matibabu na uchunguzi zaidi.

Amesema chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi na kwamba jeshi hilo limetoa wito kwa madereva wote kuendesha magari kwa kuchukua tahadhari hasa katika maeneo yenye kona na kufata sheria za usalama barabarani.




Source: Mwananchi
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages