Breaking

Saturday 13 August 2022

ZIARA YA RAIS SAMIA YALETA NEEMA NJOMBE



MWENYEKITI wa Jumuiya ya Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Mkoa wa Njombe Bi.Scolastika Kevela amemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa ziara yake ndani ya mkoa huo iliyoamsha ari ya wananchi kufanya kazi kwa bidii Ili kujiletea maendeleo.

Bi. Scolastika amebainisha hayo mkoani humo muda mfupi baada ya Rais Samia kuhitimisha ziara ya siku mkoani humo ambapo Mwenyekiti huyo wa UWT na wananchi wa Mkoa huo wamemwambia Rais Samia kuwa kwa ujio wake mkoani humo amewafuta kwa kitambaa cheupe.

" Ukweli Rais Samia ametuheshimisha sana ameufanyia mkoa wetu mambo makubwa, ujenzi wa Soko, Hospitali ya akina mama na watoto, Barabara, na kuweka ruzuku katika mbolea hivyo kupelekea bei kushuka, tuseme nini zaidi ya kumwambia kuwa ametufuta kwa kitambaa cheupe" amesema Bi. Scolastika

Amesema wao kama wana UWT na wananchi wa mkoa huo kwa pamoja wamefurahishwa na ziara yake mkoani ambayo pia ameitumia kutangaza ujio wa pili wa filamu ya Royal Tour akiita kama 'Hidden Tour' itakayoshirikisha vivutio vilivyopo katika mikoa ya nyanda za juu kusini.

"Tunaamini kupitia filamu hiyo mikoa yetu ya Kusini ukiwemo huu wa Njombe utajulikana kimataifa baada ya vivutio vyake na fursa mbalimbali za uwekezaji zilizomo ndani yake kuonyeshwa kupitia filamu hiyo" amesisitiza Bi. Scolastika

Amesema wananchi wa mkoa huo kwa pamoja wanaamini kupitia ziara yake hiyo kasi ya wananchi kufanya kazi itaongezeka baada ya kuona juhudi anazozifanya kuwaletea maendeleo huku akisisitiza kuwa kwa umoja wao kama wana Njombe watahakikisha kuwa wanasimama naye hadi atakapomaliza vipindi vyake viwili vya uongozi.

"Tunampongeza kwa kuja mkoani kwetu, sisi kama wanawake wa CCM tunaona kazi kubwa na nzuri anayoifanya kuleta maendeleo nchini, ujio wake katika mkoa huu utazidi kuamsha ari ya wananchi kufanya kazi ili kuunga mkono juhudi zake za kutuletea maendeleo wananchi wake" amesema Bi. Scolastika

Aidha amesema katika ziara yake hiyo ambapo pia ameagiza kufunguliwa shule ya awali ndani jengo la soko kubwa la mkoani hapo, ni dhahiri ameonyesha kuwajali wanawake wanaofanya biashara zao mahali hapo na watoto wao huku wakimshukuru kwa ujenzi wa soko hilo lililomaliza kabisa changamoto kwa wafanyabiashara wa mkoa huo.

Mbali na uzinduzi wa jengo hilo katika ziara hiyo, Rais Samia pia amezindua Barabara yenye urefu wa Kilomita 107 kutoka Njombe hadi Makete sambamba na jengo la kutolea huduma kwa wakina mama na watoto ambalo ujenzi wake unakwenda kutatua changamoto ya awali iliyokuwepo.

Aidha Rais Samia Akizungumza na wananchi wa mkoa huo katika Uwanja wa Sabasaba kwa kutambua faida ya zao la Parachichi linalolimwa kwa wingi mkoani humo, amewataka wakulima kuacha kuwauzia madalali maparachichi ambayo hayajakomaa kwa kuwa yanaenda kutua soko le zao hilo nje ya nchi.

Pamoja na hilo alisema Serikali itajenga viwanda viwili vikubwa mkoani humo ili wananchi waweze kuuza mazao yao huku akiahidi kutoa nyongeza ya ruzuku ya mbolea kwa ajili ya kuwawezesha wakulima kununua Kwa bei nafuu, suala lililopokelewa vyema na UWT Mkoa huo.

Akizungumzia hilo, Mwenyekiti huyo wa UWT Mkoa wa Njombe amemshukuru Rais Samia na kusisitiza kuwa Kwa niaba ya wananchi wa Mkoa huo watetekeleza agizo hilo Ili kulinda thamani ya zao hilo la kimkakati kwa Taifa.

'Sisi wanawake wa CCM wa Mkoa huu wa Njombe, tutaendelea kuwa naye bega kwa bega na kumuunga mkono katika utekelezaji wa majukumu yake ya kuwaletea maendeleo watanzania na zaidi akasema kuwa uongozi wake unaonyesha mfano mzuri kwa viongozi wengine ndani na nje yaa nchi" amesema Mama Kevela

Amewataka watanzania kwa umoja wao kuendelea kumuombea dua njema wakati wote ili aendelee kuwatumikia na kuwaletea maendeleo huku akisisitiza kuwa kutokana na uongozi wake anaamini watanzania wote watazidi kumuunga mkono.

Aidha mbali na kuzindua miradi mbalimbali mkoani humo, Rais Samia pia amesisitiza kuwa Serikali inaendelea kuuboresha miradi mbalimbali yenye nia ya kupunguza changamoto za wananchi huka akiwasisitiza kushiriki katika zoezi la sensa linalotarajiwa kufanyika Agosti 23 Mwaka huu.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages