Breaking

Tuesday 21 February 2023

JAMAA AKUTWA AMEJINYONGA KANISANI



Waumini wa Kanisa Katoliki la Mtakatifu Kalemba, Wilaya ya Bushenyi, Uganda waliamkia tukio la kushtua baada ya mwili wa mwanamume kupatikana ukining'inia kanisani.

Marehemu, Geoffrey Kigundu mwenye umri wa miaka 23, alipatikana amejinyonga Jumapili, Februari 19, kwa sababu ambazo bado hazijatambuliwa.

Kulingana na katekista wa kanisa hilo, Tukore Topista alishtuka baada ya kupata maiti ya Kigundu ikiwa inaning’inia kanisani wakati alikuwa amekwenda kujiandaa kwa Misa.

Topista anasema mwili huo ulikuwa katika sehemu ya kanisa hilo ambayo bado haijamalizwa kujengwa, na waliripoti kisa hicho katika Kituo cha Polisi cha Kizinda ambao walichukua mwili huo.

"Tulipata mwili wa mtu ukining'inia katika sehemu ambayo haijakamilika ya kanisa na hii ilishangaza sana. Tuliripoti suala hilo kwa polisi ambao walikuja na kuuchukua mwili huo. Hii ilivuruga maandalizi yetu ya Misa yetu ya Jumapili," alisema Topista kama alivyonukuliwa na gazeti la Daily Monitor.

Msemaji wa polisi wa Bushenyi, Marcial Tumusiime alisema kuwa mwili huo haukuwa na majeraha yoyote na ulikuwa ukining'inia kwenye kamba ya nailoni uliofungwa kwenye mbao.

Wakazi walisema marehemu alikuwa mfanyakazi wa kawaida ambaye siku ya Jumamosi, alimwomba mwajiri wake amlipe ili arejee nyumbani.

Mwajiri wake alimlipa na kisha aliondoka akisema anakwenda kuchukua bodaboda ili kumpeleka hadi kwenye steji ya basi lakini alikosa kurejea hadi Jumapili asubuhi wakati mwili wake ulipatikana.

Marehemu pia anasemekana alikuwa na msongo wa mawazo na alipiga simu zisizokuwa za kawaida.

Mwili wa marehemu ulipelekwa katika Hospitali ya Kimataifa ya Kampala Ishaka kwa uchunguzi wa maiti.

Chanzo: Tuko News
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages