Breaking

Tuesday 21 February 2023

WATANO WAKAMATWA KWA KUJIHUSISHA UTOAJI LESENI ZA UDEREVA, NAMBA ZA MAGARI NA PIKIPIKI KINYUME CHA SHERIA




Watu watano wanatuhumiwa kwa kujihusisha na utoaji leseni za udereva na namba za magari na pikipiki (Plate number) kinyume cha sheria.

kupitia taarifa iliyotolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, Kamishna msaidizi wa Polisi Allan Bukumbi ameeleza kuwa Mnamo tarehe 16.02.2023 majira ya saa 09:00hrs Jeshi la Polisi Mkoa wa Iringa lilipata taarifa kuwa huko maeneo ya mtaa wa Mahiwa, Kata ya Gangilonga, Manispaa na Mkoa wa Iringa kuna wafanyabiashara wa maduka yaliyopo mkabala na Ofisi za Mamlaka ya Mapato Tanzania- TRA ambayo yanajihusisha na vifaa vya maofisini wanashirikiana na baadhi ya Maofisa wa TRA kutoa leseni za udereva, kubadilisha kadi za umiliki wa vyombo vya moto bila kufuata utaratibu uliowekwa kisheria.

Katika mahojiano watuhumiwa hao walikiri kuwa wanashirikiana na Upendo Msigwa, miaka 32, mkristo, mkazi wa Mawelewele, msaidizi wa ofisi TRA na Chali Chaliga, miaka 28, mkristo, mkazi wa Donbosco, dawati la leseni TRA ambao ni watumishi wa TRA Mkoa wa Iringa kwa kutoa leseni na kuwapa wananchi bila kufuata utaratibu wa kisheria.

Kamanda bukumbi amewaeleza wananchl kuwa Jeshi la Polisi Mkoa wa Irnga linaendelea kuwatafuta wenye leseni hizo za udereva na wamiliki wa namba za magari (Plate number) kwa kosa la kula njama na kujipatia leseni na namba bila kufuata mfumo uliowekwa kwa mujibu wa sheria.

Hata hivyo Kamanda Bukumbi amesema Upelelezi unaendelea na watuhumiwa watafikishwa mahakamani baada ya upelelezi kukamilika.

Aidha, Kamanda Bukumbi alimalizia mazungumzo hayo kwa kutoa wito kwa wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi katika kutoa taarifa kwa wakati zinazohusu viashiria vya uhalifu na wahalifu wakati wote.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages