Breaking

Wednesday 1 March 2023

WAZIRI MKUU ATOA MAAGIZO UWANJA WA MKAPA

 WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameiagiza Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kuanza haraka ukarabati wa Uwanja wa Mpira wa Miguu wa Benjamin Mkapa ili ukidhi mahitaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika CAF baada ya kuufanyia ukaguzi hivi karibuni.


Ametoa agizo hilo leo (Jumatano, Machi 1, 2023) jijini Dar es Salaam alipotembelea kukagua hali ya uwanja huo baada CAF kutaka ufanyiwe marekebisho katika baadhi ya maeneo

“Ili mradi CAF wametupa onyo, ni onyo ambalo wametupa na muda wa kufanya marekebisho na muda huo waliotupa ni lazima tuanze jambo ndipo waridhie mambo mengine yaendelee, nimekuja kuwaambia msiruhusu uwanja huu umefungwa na CAF na kuzipeleka timu zetu zikacheze ugenini”

Amesema kuwa kwa kuwa CAF wameleta orodha ya makampuni yenye uwezo wa kufanya ukarabati wa kiwango cha juu hivyo Wizara itangaze zabuni ikiwezekana hata kwa mfumo wa ‘Single Source’ ili kazi ya awali ianze kufanyika katika maeneo ya kubadilishia nguo, vyoo, milango na bechi la ufundi

“CAF wakija hapa wakitukuta tunaendelea na kazi, wanaweza kuruhusu michezo mingine ichezwe ikiwa timu zetu zitafuzu katika hatua za mbele tofauti na ambayo wameiruhusu sasa, tunahitaji haya marekebisho yafanyike kuanzia sasa, Huu ni uwanja wa Taifa na zipo nchi za jirani ambazo zimeamua kuutumia uwanja huu”

Katika hatua nyingine Mheshimiwa Majaliwa kufanyike mapitio ya idadi ya mechi zitakazokuwa zinaruhusiwa kutumia uwanja huo kwa kupunguza idadi ya mechi zinazochezwa kwa lengo la kutunza uwanja huo ikiwemo sehemu ya kuchezea.

“Wizara, Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na Bodi ya ligi fanyeni mapitio ya mechi zinazopaswa kuchezwa uwanja wa Benjamin Mkapa, Tunao uwanja wa uhuru na hata Azam Complex muda mwingi havitumiki pelekeni michezo mingine huko, hapa chagueni mechi ambazo zinaingiza mashabiki wengi”

Aidha, Waziri Mkuu ametoa wito kwa Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kushirikiana na Halmashauri kutenga maeneo kwa ajili ya ujenzi wa viwanja vya michezo

“Wizara kaeni na TAMISEMI muone namna ya kuwa na viwanja, tunakabiliwa na upungufu wa viwanja vya mazoezi, Wizara lazima

mtembelee maeneo yote katika majiji na muone wapi panafaa kuongeza nguvu ili mjenge hivi viwanja”

Kwa upande wake, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Balozi Pindi Chana amesema kuwa mechi ambazo zitachezwa kabla ya ukarabati ni katika ya Simba vs Vipers, Yanga vs Real Bamako, mechi ya South Sudan na mechi nyingine ni Timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars)

Naye, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Said Yakubu amesema maeneo waliyoelekezwa na CAF kuyafanyia maboresho ni eneo la kuchezea (Pitch), Benchi ya ufundi, vyumba vya wachezaji na waamuzi, Ukumhbi wa mikutano ya waandishi wa habari.

Maboresho mengine ni kubadili eneo la waandishi wanapokaa wakati wa mechi, kubadili muonekano wa viti sehemu ya VIP, kutenga chumba maalumu kwa ajili ya marejeo ya picha (VAR Room), kubadili Taa uwanjani na kuboresha uwezo wa jenereta kwenye uwanja.

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia langolahabari@gmail.com au WhatsaApp: + 255 621 615 613 au +255 621 896 990

Pages